Mbunge wa viti maalumu CCM mkoa Kagera, Bernadeta Mushashu ametoa vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 3 ambavyo ni matofali, saruji pamoja na fedha kwaajili ya ujenzi katika shule ya sekondari Hamugembe iliyopo manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.

Mbunge huyo amesema kuwa elimu ni chachu ya maendeleo kwa Watanzania na kuongeza kuwa ikiwa ni wiki ya maadhimisho ya siku ya wanawake duniani kwa upande wa mkoa wa Kagera wataiadhimisha kwa kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo.

Kwa upande wake mkuu wa shule ya sekondari Hamugembe Mwalimu, Melania Buberwa amesema kuwa shule hiyo ina wanafunzi 437 ambapo upungufu wa vyumba vya madarasa ni vyumba vitano na kueleza kuwa mchango alioutoa mbunge huyo utasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza uhaba wa vyumba vya madarasa kwa kumalizia ujenzi unaoendelea.

Naye diwani wa Kata hiyo, Muhajj Kachwamba ameishukuru serikali ya awamu ya tano kwa kazi kubwa inayoifanya ya kuhakikisha maendeleo ya wananchi yanasonga mbele pamoja na kumshukuru mbunge huyo kwa mchango mkubwa wa vifaa vya ujenzi.

Baadhi ya wanafunzi wamemshukuru mbunge huyo kwa kutoa msaada huo katika shule hiyo, ambapo wamesema changamoto kubwa wanazokumbana nazo watoto wa kike katika shule hiyo ni suala zima la vyoo.

Jumaa Aweso awashukia wataalamu wa maji, 'Msitudanganye sisi viongozi'
Tanesco yatoa mafunzo kwa makundi maalum kwa watu wenye ulemavu