Mbunge wa viti maalumu wa chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani wa Kagera, Bernadeta Mushashu ametoa msaada wa viti mwendo 10 vya kutembelea (wheelchairs) kwa watoto wenye ulemavu wa viungo, Sukari, Sabuni, Soda vyenye thamani ya shilingi laki saba katika shule ya msingi Mugeza Mseto katika kuadhimisha siku ya wanawake duniani ambayo hufanyika kila ifikapo tarehe 8 ya mwaka.
 
Akizungumza mara baada ya kutoa msaada huo, Mushashu amesema kuwa wanawake wa Manispaa ya Bukoba wameona kuwa si busara kusherekea siku yao bila kufika kuwaona watoto hao wenye mahitaji maalumu.
 
Amesema kuwa watoto wenye ulemavu ni sawa na watoto wengine hivyo jamii haipaswi kuwatenga kwa kuwaona hawana maana na kuitaka jamii na wazazi wenye watoto ambao ni walemavu kuacha mila potofu za kuwaficha watoto wao na kuwanyima haki zao za kupata elimu.
 
“Nawashukuru wazazi ambao hawakuwaficha na kuwaleta kupata elimu, niwashukuru pia walimu kwa huduma nzuri ya kuwatunza watoto hawa maana ni kazi kubwa kwa changamoto walizonazo, lakini pia niwaombe watoto ambao mna uwezo wa kutembea wasaidieni wenzenu wasioweza kutembea, Mimi kama mbunge changamoto zote zilizopo hapa nazipeleka kwa waziri ili zifanyiwe kazi.”amesema Mushashu.
 
Kwa upande wake mwalimu mkuu msaidizi wa shule hiyo ya Mugeza Mseto, Joyce Rubozi amesema kuwa watoto hao wanakabiliwa na changamoto kubwa hasa wenye ulemavu wa viungo ambao idadi yao ni zaidi ya 60 lakini viti mwendo kwaajili yao ni 10 ambavyo pia sio salama suala linalopelekea watoto hao kupata adha kubwa.
 
Wakitoa shukrani zao kwa mbunge huyo watoto hao wamemuomba mbunge huyo kufikisha changamoto zao kwa waziri wa elimu ili kuweza kuwasaidia kutatua changamoto wanazokumbana nazo.
 
Shule hiyo ya Mugeza Mseto ipo Kata ya Kahororo Manispaa ya Bukoba inajumla ya zaidi ya wanafunzi 750 ambao wanafunzi zaidi ya 150 kati yao ni walemavu wa aina mbalimbali hivyo jamii inaombwa kuendelea kuwasaidia watoto hao ili kuweza kuzifikia ndoto zao.

Kupungua kwa bei ya bidhaa kwanusuru mfumuko wa bei.
Jela miaka 11 kwa kumkeketa mwanaye jijini London