Rais Uhuru Kenyatta ameamuru wabunge 7 wa chama cha Jubilee Nchini Kenya wavuliwe vyeo walivyoshikilia katika kamati za Bunge.

Duru za kisiasa nchini humo zinadai kuwa wabunge hao walipokea barua kutoka kwa Chama cha Jubilee wakitakiwa kuelezea umuhimu wao katika vyeo hivyo ilhali walimkaidi Rais na pia kusaliti chama hicho tawala.

Kando na Mwakilishi wa Kike katika kaunti ya Laikipia, Catherine Waruguru wengine walioadhibwa ni David Gikaria (Mbunge Nakuru Town Mashariki), Katoo Ole Metito (Kajiado Kusini), Ali Wario (Bura), Kareke Mbiuki (Maara), Rashid Mwashetani (Lunga Lunga) na William Kisang’ (Marakwet Magharibi).

Chama hichi kilichukua hatua hiyo sababu wabunge hao walichaguliwa kupitia tiketi yake lakini sasa wamehamia United Democratic Alliance (UDA), ambacho ni chama kinachohusiana na Naibu Rais William Ruto.

Wabunge hao wamepewa siku saba kujitetea kwa kutoa sababu za kuridhisha la sivyo watapoteza vyeo vyao.

“Kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za 176 (1) na 176 (2) unafahamishwa kuwa Chama cha Jubilee Party kilikuteua kuwa katika Kamati ya Idara ya Habari na Teknolojia ya Mawasiliano. Kwa hivyo unapewa siku saba kujibu kabla ya kuondolewa kwenye Kamati,” ilisoma moja barua hiyo.

Kiongozi wa walio wachache katika Bunge la Kitaifa, Emmanuel Wangwe, alisema iwapo wabunge hao hawatatoa majibu ya kuridhisha, basi chama kitakuwa huru kuwaondoa katika nyadhifa hizo. Kwa upande wake kiongozi wa walio wengi katika Bunge la Kitaifa, Amos Kimunya, amesema, marekebisho katika kamati za Bunge ni mchakato endelevu wa kuzifufua na kuhakikisha uongozi wao unawiana na wanachama.

Kaligraph Jones kurejea shuleni
TFS yaja na suluhu