Mbunge wa Kawe (CHADEMA), Halima Mdee amesema kuwa hawezi kuogopa kauli ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama cha mapinduzi (CCM), Humphrey Polepole kuwa katika uchaguzi mkuu wa 2020 hawezi kuchaguliwa tena.

Mdee amesema hayo katika mahojiano maalum na amefunguka kuwa hakuna diwani wala Mbunge wa CHADEMA ambaye amekwenda kuomba kujiunga na CCM kama Polepole anavyodai.

“Hakuna kiongozi anayeomba kujiunga na CCM, huyu Polepole anatetea kibarua chake tu”, amesema Mdee.

Akizungumzia kuhusu viongozi wa upinzani kuhamia CCM amesema kuwa wanasiasa pia ni binadamu na sio malaika hivyo wapo waaminifu na wasiokuwa waaminifu na kinachopelekea yote hayo ni tamaa na ugumu wa maisha.

“Kwenye kazi hii huwezi kukwepa kutofanya kazi na watu wasiokuwa waaminifu na kinachowashinda kukaa upinzani ni uoga hawawezi mapambano wakitishiwa tu kidogo wanahama na sio kwamba wanaomba”, amesema Mdee.

Katika mahojiano maalum aliyofanyiwa na kituo cha EATV 28, 2018 Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Humphrey Polepole alisema kuwa kuna baadhi ya wabunge wa vyama vya upinzani hata wasijisumbue kujiunga na CCM kwani hawatopokelewa na chama hicho na watafute kazi za kufanya ifikapo mwaka 2020 kwakuwa utakuwa ndio mwisho wao kisiasa.

“Kuna wabunge wameshaomba kujiunga na CCM hasa wa Dar es salaam, lakini kutokana na mienendo yao tumewakataa kwani huwezi tukana maendeleo wakati unatumia hivyo hivyo unavyopingana navyo”, amesema Polepole.

Ali Kiba: Hela ni wimbo wa kuenzi marehemu
Mkoa watenga bajeti ya taulo za kike