Aliyekua beki na nahodhwa klabu ya Arsenal Per Mertesacker, anaamini Arsene Wenger bado ana nafasi ya kuwa meneja wa klabu kubwa barani Ulaya, licha ya mpaka sasa kutopata nafasi hiyo, tangu alipoachana na The Gunners mwishoni mwa msimu uliopita.

Mertesacker, ambaye alitangaza kustaafu soka mwishoni mwa msimu uliopita akiwa na Arsenal ya jijini London, ameonyesha imani hiyo kwa aliyekua bosi wake, huku taarifa zikieleaa kuwa, huenda babu Wenger akatangazwa kuwa mkuu wa benchi la ufundi la mabingwa wa soka nchini Ujerumani FC Bayern Munich, endapo meneja wa sasa Niko Kovac atatimuliwa.

Mertesacker mwenye umri wa miaka 34, amesema Wenger bado ana uwezo mkubwa wa kufundisha soka, tena kwenye klabu zenye umahiri wa kupambana na yoyote duniani, hivyo hatoshangazwa kumuona akirejea kwenye moja ya klabu bingwa barani Ulaya.

“Sina shaka kabisa na mzee huyu, anajua anachokifanya pindi anapokua kazini, binafsi ninasubiri kusikia akianza kazi katika moja ya klabu kubwa hapa Ulaya, wakati wowote.”

“Sijajua ni wapi atakapoelekea, lakini kwa namna ninavyomfahamu Wenger, pamoja na ukimya wake lakini kuna kitu kwa sasa anakitafuta ili afanikishe mpango wa kurejea kwenye majukumu ya ukufunzi wa soka.

“Meneja kama huyu hawezi kukaa kipindi kirefu bila ya kuwa na kazi, ninaamini kuna baadhi ya klabu zimeshajaribu kumshawishi lakini amezigomea, kutokana na malengo aliyojiwekea.”

“Ninapendezwa sana na ukufunzi wa Arsene Wenger, anajua namna ya kutengeneza kikosi cha ushindani, nimethubutu kusema hivi kwa sababu nimekua chini yake tangu nilipojiunga na Arsenal mwaka 2011.”

Mertesacker alicheza michezo 156 chini ya utawala wa wenger, baada ya kusajiliwa akitokea Werder Bremen ya nchini kwao Ujerumani, na alitwaa mataji matatu ya komnbe la FA.

Wenger, amekua akitajwa katika harakati za kufikiriwa na viongozi wa FC Bayern Munich, kufuatia hali kumuendea kombo meneja wa sasa wa klabu hiyo Niko Kovac, ambaye ameanza kuonyesha huenda akashindwa kufikia malengo yaliyowekwa.

Serikali yazionya NGOs, yaanza kuzichunguza kimyakimya
Majaliwa achukizwa wanafunzi 72 kupewa ujauzito Nyang’hwale, atoa maagizo mazito