Aliyekuwa Meya wa Jiji la Arusha Kalisti Lazaro amejiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kupokelewa na Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM.

Lazaro ameeleza kuwa amefikia uamuzi huo baada ya kupitia wakati mgumu akiwa katika Wadhifa wake wa Meya wa Jiji la Arusha, ameyasema hayo leo alipofika katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM Lumumba jijini Dar es salaam.

Ameeleza kuwa Vitisho vya mara kwa mara ikiwamo dhidi ya uhai wake ndio vimepelekea kujivua nafasi zake zote katika Chadema na kujiunga na CCM, amepokea barua za maonyo mara kadhaa kutoka Uongozi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Barua hizo zilimtaka kutokutoa ushirikiano na Viongozi wa Serikali ambao anatakiwa kufanya nao kazi ngazi ya Mkoa na Wilaya na kutompongeza hadharani John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri ambayo ameifanya Nchini ikiwamo katika Mkoa wa Arusha.

Lazaro pia amechukizwa na Chama chake kujitoa katika uchaguzi huku akiita kitendo hicho uvunjaji wa demokrasia ambacho ndani ya masaa mawili uamuzi wa Kamati Kuu ya Chadema iliwanyima mamilioni ya wapenda demokrasia haki ya kushiriki katika Uchaguzi huu wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji.

Amesema sasa yuko tayari kuchapa kazi ya wananchi akiwa ndani ya Chama ya Mapinduzi na kwamba yuko tayari kwa maelekezo ya kazi kutoka Uongozi wa CCM.

Hivyo basi kwakujiunga na CCM amejiuzuru nafasi ya Udiwani, Umeya wa Jiji la Arusha, Uenyekiti wa Mameya na Madiwani wote wa Chadema Nchini na Ujumbe wa Kamati Kuu ya Chadema.

Video: Meya Kinondoni azindua mashindano ya kuvua
TECMN yaipongeza Mahakama ya rufani Tanzania