Mshambuliaji wa Yanga, Malimi Busungu, ametoweka katika kikosi hicho baada ya kumalizika kwa mchezo dhidi ya Simba huku akiwa hajatoa taarifa yoyote kwa uongozi wa klabu hiyo.

Taarifa zinaeleza kuwa, mshambuliaji huyo ameamua kutoweka kutokana na kuona hapewi nafasi katika kikosi hicho tangu msimu ulipoanza, hivyo ameamua kujiongeza zaidi.

Chanzo kutoka Yanga kimeeleza kuwa, Busungu alikuwa na mpango huo kabla ya mchezo dhidi ya Stand United, lakini akaja kufanya utekelezaji wake baada ya mpambano na Simba ambapo aliamua kuzima simu yake kabisa.

“Busungu alikuwa na mipango ya kuondoka tangu tulipomaliza mechi yetu na Stand United ambapo aliamua kuondoka rasmi baada ya kumalizika mechi na Simba, kisa kikiwa ni kukosa nafasi ya kucheza.

“Baada ya kutoweka hakuwa akipatikana na simu yake ilikuwa imezimwa kila alipokuwa akipigiwa, hivyo kwa taratibu za kazi mtu akitoweka kazini siku tatu bila ya mawasiliano ajira yake inakuwa ameisitisha mwenyewe mkataba kwa kuwa hayupo klabuni zaidi ya wiki sasa,” kilisema chanzo hicho.

“Hivi karibuni simu yake ilipatikana na nimeongea naye lakini amesema hawezi kurejea kwa sasa kufanya mazoezi na Yanga kwa kuwa bado anaumwa, pia ana matatizo ya kifamilia ambayo yanamzuia kuja kujiunga na timu.

“Ameondoka bila ya kuaga na tayari barua imeshafikishwa kwa uongozi juu ya kufanya maamuzi yake kwani hata benchi la ufundi limeshindwa kutoa maamuzi yoyote,” kiliongeza chanzo kingine.

Hata hivyo, alipotafutwa Katibu Mkuu wa Yanga, Baraka Deusdedit, amekiri kutokea kwa tukio hilo ambapo amesema: “Ni kweli jambo hilo lipo lakini lipo kiofisi zaidi na aliomba ruhusa na iwapo kuna watu wanasema hajaomba ruhusa basi waulize hao hao.”

Alipotafutwa Kocha wa Yanga, Hans Pluijm kuzungumzia juu ya suala hilo, alisema: “Busungu ana matatizo binafsi ambayo yatatatuliwa ndani ya uongozi, hivyo siwezi kuzungumzia.”

Alipotafutwa Busungu kuweza kuzungumzia suala hilo simu yake ilikuwa inaeleza inatumika kila wakati na hata alipotumiwa ujumbe mfupi hakujibu.

Zeben: Tulikuwa Na Mchezo Mzuri, Tuliwazidi Kila Kitu Yanga
Mkwasa Aukubali Mziki Wa Msimbazi, Alaani Umimi