Mfumuko wa bei wa Taifa umepanda kwa asilimia 0.2 baada ya kuongezeka hadi asilimia 3.6 toka asilimia 3.4 kwa mwaka ulioisha mwezi september 2019 kutokana na kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma.

Akizungumza na waandishi wa Habari Jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi wa sensa ya watu na takwimu za jamii Ruth Davison amesema kuongezeka kwa mfumuko huo kumechangiwa na kupanda kwa bei za bidhaa za vyakula kwa kipindi kilichoisha mwezi oktoba 2019 ikilinganishwa zile za mwezi oktoba 2018.

“Ongezeko hili la asilimia 0.2 limechangiwa na kupanda kwa bei za vyakula kwa kipindi kilichoisha mwezi oktoba 2019 ikilinganishwa zile za mwezi oktoba 2018 tukumbuke kwamba hapo awali tulikua na asilimia 3.4 na sasa ni asilimia 3.6,” amebainisha Ruth.

Amesema mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioisha mwezi oktoba 2019 umeongezeka hadi asilimia 5.1 kutoka asilimia 4.0 kwa mwaka ulioisha mwezi september 2018 na kwamba hatua hiyo inatokana na matumizi mengi ya bidhaa hizo.

Aidha amesema mfumuko wa bei kwa bidhaa na huduma ambazo hazijumuishi chakula na nishati kwa mwezi Oktoba – 2019 umepungua hadi asilimia 2.6 kutoka asilimia 2.7 Septemba, 2019.

“Fahirisi za bei kati ya mwezi Septemba, 2019 na mwezi Oktoba, 2019 zimepungua kwa asilimia 0.1 ambapo badiliko ni sawa na lilivyokuwa kati ya mwezi Agosti, 2019 na mwezi Septemba 2019,” amefafamua Bi. Minja.

Kwa upande wa hali ya mfumuko wa bei kwa baadhi ya nchi za afrika mashariki ikiwemo Kenya ambayo mfumuko wa bei kwa mwaka ulioisha mwezi oktoba 2019 umeongezeka hadi asilimia 4.95 kutoka asilimia 3.83 kwa mwaka ulioisha mwezi septemba 2019.

“Hivyo basi mnaweza mkajionea wenyewe hali halisi ilivyo kwa viwango vinatofautiana kwa asilimia 1.12 kwa mwaka ulioisha mwezi oktoba mwaka huu kuongezeka hadi asilimia 4.95 kutoka asilimia 3.83 kwa mwaka ulioisha mwezi septemba,” amefafanua zaidi Bi. Davidson.

Ofisi ya taifa ya takwimu (NBS) ni taasisi ya umma iliyoanzishwa kwa sheria ya Takwimu ya mwaka 2015 iliyopewa mamlaka ya kutoa, kusimamia na kuratibu upatikanaji wa taarifa za kitakwimu nchini ikiwa ni pamoja na takwimu za mfumuko wa bei kwa ajili ya matumizi ya serikali na wadau wengine.

Serikali yafuta mamlaka za maji safi na usafi wa mazingira
Video: Ni maswali 4 kwa Jafo, ageuka, Upimaji Virusi HIV kupitia mate waja