Rais wa zamani wa Madagascar, Hery Rajaonarimampianina, amedai kuwa chama chake kimegundua kuwepo kwa dosari nyingi za uchaguzi katika uchaguzi uliofanyika wiki hii, matamshi ambayo yanazua wasiwasi wa kuzuka kwa maandamano na kupingwa kwa matokeo.

Matokeo ya awali kutoka katika baadhi ya vituo yanamuweka Rais Hery katika nafasi ya tatu nyuma ya wagombea wengine, Andry Rajoelina na Marc Ravalomanana, ambao wote waliwahi kuwa viongozi wa taifa hilo kwa nyakati tofauti.

Akizungumza jijini Antananarivo, amesema kuwa uchaguzi huo ulikuwa na dosari za kiufundi ikiwemo orodha ya watu waliosajiliwa kimakosa, vitisho na uwepo wa karatasi ambazo tayari zilikuwa zimepigwa kura.

Aidha, kiongozi huyo amesema kuwa hawatakubali kuona wananchi wananyang’anywa haki yao ya msingi kupitia kura waliyopiga.

 

Hata hivyo, matamshi ya Rais Rajaonarimampianina yanakinzana na yale ya waangalizi wa Umoja wa Ulaya na Umoja wa Afrika waliotoa taarifa za awali kueleza kuwa uchaguzi huo ulikuwa huru na hapakuwa na dosari kubwa

Ripoti ya ukeketaji Afrika yatoa picha mpya, Tanzania yachomoza
Video: JPM awafukuza Tizeba, Mwijage, Samia aionya Takukuru kuwakumbatia wala rushwa