Mwanaume mmoja aliyekuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Nanyuki nchini Kenya amedaiwa kugeuka mbogo na kumuua mgonjwa mwenzake, Ronney Mutuma, Jumamosi iliyopita.

Mutuma mwenye umri wa miaka 42, aliyekuwa akitibiwa katika hospitali hiyo, alifikwa na umauti siku moja baada ya mgonjwa huyo kumpiga na kitu kizito kichwani na baadaye kuwajeruhi watu wengine wanane wakiwemo wauguzi.

Waziri wa Afya wa Kaunti ya Nanyuki, Joseph lenain amesema kuwa Mutuma aliuawa na mgonjwa aliyekuwa akitibiwa shinikizo la damu (hypertension) katika hospitali hiyo.

Ameeleza kuwa katika purukushani za shambulizi hilo, mtu huyo mwenye umri wa miaka 48 aliwajeruhi pia wagonjwa wengine sita na wauguzi wawili.

“Marehemu alikuwa akitibiwa kutokana na maradhi ya kisukari na alikuwa amelazwa kwa siku tatu katika hospitali hiyo ya Kaunti yetu,” Citizen ya Kenya inamkariri Lenai.

Mkuu wa Polisi wa eneo hilo, OCPD Kizito Mutoro ameeleza kuwa uchunguzi wa tukio hilo umeanza na kuwataka wafanyakazi wa hospitali kuwa makini na wagonjwa wa aina hiyo.

Wananchi wachoma kanisa, wadai linawaletea pepo wachafu
Video: Fatma Karume afunguka mengine kuhusu muswada, demokrasia