Mgonjwa wa kwanza kuathirika na virusi vya Corona nchini Tanzania, Isabella Mwampamba, ameaongea na waandishi wa habari leo Machi 18, 2020 jijini Arusha na kuomba msamaha.

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amefanikisha maongezi hayo alipokuwa kwenye ofisi ya mkuu wa mkoa wa Arusha Mrisho Gambo mapema asubuhi ya leo ili kupunguza taharuki kwa wananchi.

“Naomba msamaha kwa kuwa mgonjwa wa kwanza wa corona Tanzania, nimeleta taharuki nchi nzima na watu wengi waliona kama mimi ni kisababishi nipo hapa kuomba msamaha” Amesema Isabella

Amewashukuru viongozi wa dini masheikh na wachungaji kwa kumpigia simu na kumfariji, pia wauguzi wa hospitali ya mawenzi kwa kumhudumia kwa hali na mali.

“Ujumbe wangu kwa watanzania tutumie muda mwingi kuelimishana kuliko kukuza ukubwa wa ugonjwa huu, kwani upo dunia nzima na ‘kupanik’ hakusaidii isipokuwa kuchukua tahadhari”.

Waiziri Mwalimu amesema licha ya kuwa ni kweli ugonjwa upo, watanzania hawatakiwi kutaharuki na kusambaza taarifa za uongo.

Amethibitisha kuwa mgonjwa huyo anaendelea vizuri, hana homa wala mafua, na kwa watu 26 ambao wamehusika kwenye mtandao wa mama Isabella bado wapo kwenye uangalizi maalum.

Ametoa ufafanuzi kuwa kutokana na hatari ya virusi hivyo, maabara pekee inayokidhi vigezo vya kupima ugonjwa huo ni maabara kuu ambayo ipo jijini Dar es salaam, lakini serikali ipo kwenye hatua ya kusambaza vipimo vya awali kwa hospitali za mikoa.

CORONA yavunja mkataba wa John Mikel Obi
CORONA: Mtibwa Sugar waondoka Tanga