Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dkt. Bashiru Ally amesema hakuna  udikteta kwenye utawala wa awamu ya tano wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Dkt. Bashiru alisema hayo katika mahojiano Maalum na Idara ya Habari-MAELEZO ofisini kwake jijini Dar es Salaam hivi karibuni, kuhusu nidhamu na uadilifu Serikalini.

Kauli hiyo ya Dkt. Bashiru inakanusha madai ya baadhi ya wanasiasa kuwa Serikali ya sasa ni ya  kidikteta na kueleza kuwa Serikali ya Rais Magufuli ni yenye nidhamu na uadilifu kwa wananchi inaowatumikia.

Alisema lugha ya udikteta inayozungumzwa na baadhi ya watu inaashiria kuwa Watanzania hawajaafikiana juu ya namna ya kusimamiana ili anayetenda kwa nidhamu na uadilifu atukuzwe na asiyetenda kwa nidhamu na uadilifu aadhibiwe kwa mujibu wa sheria.

“Hata hii lugha inaitwa ya udikteta, mimi nikiisikiliza naona kuna kutofautiana sana tangu Rais Magufuli ameingia madarakani, juu ya namna ya kusimamiana ili wanaotimiza wajibu wao wasifiwe, watukuzwe watunukiwe na wale wasiotimiza kwa maana wanaotuangusha waadhibiwe kwa misingi na taratibu zilizowekwa”, alisema Dkt Bashiri na kukelezea upotoshwaji kuwa:

Kuna mjadala hata kama si wa kitaifa au mkubwa, lakini ukifuatilia kwenye vijiwe na kwenye vyombo vya habari unaona tunatofautiana sana katika uelewa juu ya nidhamu na uadilifu, na mimi silaumu hao wanaokwenda mbali na kusema huu sio usimamizi mzuri, bali ni udikteta.

“Mimi sikubaliani nao lakini wanatusaidia kutuambia bado tuna tatizo la kutokukubaliana na kwamba hatuna ufahamu wa pamoja juu ya hicho tunachokiita nidhamu na uadhilifu kazini.”

Alifafanua kuwa Rais Magufuli bado yupo sahihi katika uongozi wake na watanzania wamempa mamlaka ya kuongoza, hivyo ni lazima kuheshimu uongozi uliopewa dhamana na wananchi , badala ya kumkwamisha, kumdharau na kumbeza kwani yeye ndiye anayebeba mamlaka hiyo.

Dkt. Bashiru alisema hakuna mjadala na ni dhahiri kwamba mkakati wa Rais Magufuli  kwa miezi tisa aliyokaa madarakani, unajenga upya nidhamu na maadili au uadilifu hasa katika utumishi wa umma” alisema Dkt. Bashiru na kuongeza:

“Mjadala uliopo ni jinsi gani mkakati huo unatekelezwa, wapo wanaotamani Rais  aongeze kasi mara mbili na wanadhani wale wanaomkosoa wanamchelewesha katika azma yake ya kutimiza ahadi alizowaahidi Watanzania” alisema Dkt. Bashiru na kuongeza:

“Na wengine wanadhani abadilishe mkakati.Sasa itatuchukua muda kuja kupima lakini kwa mtu anayefuatilia miezi tisa inatosha kuonesha muelekeo, bado yupo  katika muelekeo sahihi.”

Akizungumzia siasa na wanasiasa, Dkt. Bashiru alisema anachelea kusema kuwa kwenye siasa kumeingia ubabaishaji kwani haridhiki na utendaji wa baadhi ya viongozi wa kisiasa.

  “Mimi sitaki kusema kwamba kwenye siasa kumeingia ubabaishaji nitaonekana labda sina nidhamu, lakini siridhiki kwa namna viongozi wetu wa kisiasa, yaani sijaridhika na utendaji wao” alibainisha Dkt. Bashiru na kufafanua kuwa:

“Siridhiki kwa namna wanavyosimamia majukumu yao kwenye taasisi zao, wengi wao wanatumia nafasi zao za uongozi, utendaji kazi wao na kauli zao kuwatenganisha wananchi na Serikali yao,  badala ya kuwaunganisha kwa pamoja.

“Na hapa asiwe anatajwa Rais peke yake kanakwamba yeye ndiye ameomba kura peke yake, bali kuna maelfu ya watu wameomba kura katika nchi hii na kupewa dhamana , hivyo watapimwa wamefanya nini katika nafasi zao miaka mitano ijayo.Wanasiasa wetu na utendaji wao na kauli zao  hasa katika  kuwatenganisha wananchi ”.

Akitoa ushauri Dkt Bashiru aliwataka wanasiasa, wasomi na vyombo vya habari wasiisaliti nchi yao badala yake watekeleza wajibu wao kwa umma ili warejesha nidhamu na uadilifu uliokosekana nchini ambazo ni tunu zilizoachwa na waasisi wa Taifa la Tanzania.

“Kwa sababu maeneo mengi ya tatizo hili tunalolisema, wahusika wakubwa ni sisi.Haingii kilaza mahakamani akawa jaji, ni mtu aliyesoma, huwi wakili, mwandishi wa habari mpaka umesoma na sasa hivi kuna muelekeo huo huwi mwanasiasa mpaka umesoma” alisema Dkt. Bashiru.

Alisema uwekezaji mkubwa wa Serikali katika elimu umewezesha kupata wasomi katika kila ngazi, kwa hiyo ni vyema wakatekeleza wajibu wao kwa nidhamu na uadilifu ili kusitokee makosa kama ya watumishi hewa na majipu.

“Mwalimu Nyerere alisema msomi akishapata neema ya kusomeshwa alafu asiwajibike kwa waliomsomesha, huo ni usaliti” alisema Dkt. Bashiru.

Dkt. Bashiru aliwataka wasomi wa kada mbalimbali kurekebishana pale wanapokiuka maadili ya taaluma zao, badala ya kusubiri kulalamika pale maamuzi yanapochukuliwa dhidi yao kwani hayo ni matokeo ya vyama vya kitaaluma kutotimiza wajibu wao.

Alisema iwapo mawakili, walimu, madaktari wakiisimamiwa vyema na vyama vyao vya kitaaluma, nidhamu na uadilifu vitarejea nchini na hivyo kufanikisha utekelezji wa mipango ya maendeleo ya nchi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Magufuli Atoa Siku Saba kwa Wizara ya Ujenzi Kulipa Deni Wanalodaiwa na NHC
Tume ya Mipango Yataka Uwekezaji Uwe na Tija na Usaidie kuibua Miradi Sahihi