Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe amesema ameunda kamati ya wanasheria kwa lengo la kupitia upya mikataba ya wasanii ili waweze kulipwa fidia zao kwani wasanii wamekuwa wakifanya kazi kubwa na makampuni mbalimbali bila kunufaika kutoka kwa makampuni hayo.

Mwakyembe amesema kwa kuanza imeunda kamati maalumu ya wanasheria kukagua mikataba yote ya mashirika na makampuni waliyoingia wasanii King Majuto na marehemu Seteven Kanumba ‘Kanumba’ na endapo kutakuwa na uonevu wowote watalipwa fidia.

Mwakyembe amefikia hatua hiyo baada ya msanii wa filamu na mchekeshaji maarufu nchini, Amri Athuman maarufu King Majuto akiomba msaada wa Shilingi laki tano (500,000) kwa ajili ya matibabu huku kuna makampuni yaliyofaidika naye kwa kuingia mikataba na kufanya naye baadhi ya matangazo ambayo mpaka sasa yanarushwa katika vyombo mbalimbali vya habari na makampuni hayo kuendelea kunufaika.

Amesema serikali imechoka kusikia vilio vya wasanii wa filamu kudhulumiwa haki zao na sasa imeunda kamati maalumu ya wanasheria kukagua mikataba yote ya mashirika na makampuni waliyoingia wasanii.

“Kwa kweli dhuluma kwa wasanii ilikuwapo kubwa sana kwa kutumia ‘middle men’ (watu wa kati), watu wenye fedha wamechezea sana Watanzania wetu. Hili limeanza kubadilika tumeanza kuwa- empower (kuwezesha) wasanii wetu kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) wasitumie middle men.“Kwa mfano vijana wetu wazuri kama kina Kanumba, amefariki kila mtu anajua ni milionea, hapana.. waliotajirika ni wengine. Leo hii mwanasanaa mzuri mzee majuto anaumwa, anaomba fedha, mimi nachanga kutoka mfuko kwangu,” alisema Dk. Mwakyembe.Alisema licha ya kwamba nusu ya mabango ya biashara na matangazo ya biashara ni ya Mzee Majuto inashangaza kuona anaomba fedha ya matibabu.

Aidha ameagiza wasanii wote ambao wanaona wameingia mikataba ya kionevu na makampuni au mashirika hayo wawasilishe taarifa zao kwa serikali.

Rais Magufuli atuma salamu za pole kwa familia ya Kandoro
Heche afunguka mazito juu ya kifo cha mdogo wake