Waliokua wawakilishi wa Nigeria kwenye michuano ya Klabu Bingwa Barani Afrika Plateau United, wameondoka Tanzania wakiwa na kumbukumbu ya shughuli iliyofanywa kiungo mshambuliaji kutoka nchini Msumbiji na klabu ya Simba SC Luis Miquissone, katika mchezo miwili iliyozikutanisha timu hizo.

Plateau United waliondoshwa kwenye michuano hiyo kwa jumla ya bao moja kwa sifuri lililofungwa kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza mjini Jos-Nigeria, kabla ya kucheza mchezo wa mkondo wa pili jijini Dar es salaam Jumamosi (Desemba 05).

Kabla ya kuondoka nchini kurejea kwao Nigeria, beki wa kati wa Plateau United, Denis Nya, alizungumza na baadhi ya vyombo vya habari na kusema kuwa Simba walicheza vizuri, lakini mchezaji aliyewasumbua sana ni aliyevaa jezi namba 11 (Luis Miquissone), na alifanya hivyo katika michezo yote miwili waliocheza.

Alisema Miquissone aliwasumbua katika michezo yote miwili, wakiwa kwao Nigeria pamoja na mchezo wa juzi ambao aliweka wazi kama wasingekuwa makini kuziba njia zake wangefungwa tena.

“Ulikuwa mchezo wa ushindani kwa kila timu, tulikuja kutafuta matokeo, ila bahati haikuwa kwetu, lakini mchezo ulikuwa mzuri tunawapongeza Simba kwa kusonga mbele katika michuano hii.”

“Wachezaji wote walifanya majukumu yao ila aliyevaa jezi namba 11, alikuwa hatari sana kwetu kwa sababu ametengeneza nafasi nyingi, lakini ndivyo hivyo kwenye soka kuna matokeo matatu, tunakubali na sasa tunarejea nyumbani,” alisema Nya.” Alisema Nya.

Simba SC itakutana na FC Platinum ya Zimbabwe iliyoitoa Costa do Sol ya Msumbuji kwa jumla ya mabao 4-1 ikiwa ni baada ya mchezo wa awali ugenini kushinda 2-1 na ule wa marudiano nyumbani kuibuka na ushindi 2-0 Jumamosi iliyopita.

Simba SC itaanzia ugenini katika mchezo utakaopigwa Uwanja wa Taifa wa Zimbabwe kati ya Desemba 22-23 kabla ya kurudiana kati ya Januari Januari 5-6 kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.

TAMISEMI yatoa siku 14 kuanza kutumika kwa kituo cha mabasi Mbezi Luis
Jesé Rodríguez avunjiwa mkataba PSG