Grace Mugabe, mke wa Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe amemtaka mumewe kutengua msimamo wake na kumtaja mrithi wake katika nafasi ya urais kutoka kwenye chama cha Zanu-PF ili kuondoa vita baridi inayojitokeza.

Akizungumza na wajumbe wa umoja wa wanawake wa chama hicho tawala, Mama Grace alisema kuwa hakuna ubaya kama Rais atamtaja hadharani mrithi wa kiti chake ili wajumbe wote wa chama hicho waweze kumuunga mkono mtu huyo.

Mugabe mwenye umri wa miaka 93 amepanga kugombea tena nafasi ya urais katika uchaguzi mkuu ujao hivyo kuongeza utawala wake zaidi ya miaka 37. Mugabe amekuwa rais tangu nchi hiyo ilipopata uhuru na amekuwa akishinda katika chaguzi zote.

Hata hivyo, Mugabe amewahi kunukuliwa akisema kuwa msimamo wake ni kutomtaja mrithi wa kiti chake akieleza kuwa wananchi ndio wanaotakiwa kumchagua kiongozi.

Msimamo huo wa Mugabe imedaiwa kuleta uhasama wa chini kwa chini kwa wajumbe wa chama hicho tawala, huku wajumbe wengine wakianzisha makundi ya kuwasapoti wanaowadhania kuwa wanaweza kumrithi.

Video: Spika akata, NEC yafunua, Tutanyamaza tukiwa wafu - Lissu
Dkt. Mpango awaonya wanaokwepa mashine za EFDs