Mwandishi wa habari wa Urusi ambaye ni mkosoaji mkubwa wa serikali ya nchi hiyo amekutwa ameuawa kwa kupigwa risasi nchini Ukrine alikokuwa akifanya shughuli zake za habari.

Msemaji wa Polisi nchini Ukrine, Yaroslav Trakalo amesema kuwa mwandishi huyo, Arkadi Babchenko alikutwa chumbani na mke wake akivuja damu baada ya kusikia milio ya risasi.

Mwandishi huyo aliyeuawa alikuwa akiongoza kipindi katika televisheni ya binafsi nchini Ukraine ya ATR kwa mwaka mmoja sasa na ni mkosoaji mkubwa wa Rais Vladimir Putin.

“Arkadi Babchenko aliuawa kwa kupigwa risasi tatu mgongoni mwake nyumbani kwake baada ya kutoka dukani,”amesema mwandishi wa habari mwenzake Osman Pashayev

Aidha, Babchenko amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 41 na aliondoka Urusi Mwezi Februari mwaka jana baada ya kupokea vitisho kufuatia hatua yake ya kuikosoa Urusi juu ya jukumu lake katika mgogoro wa Mashariki mwa Ukraine, akiishutumu kutoa msaada wa kijeshi kwa waasi.

Hata hivyo, msaidizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Ukraine, Anton Guerachchenko, moja kwa moja ameinyooshea kidole Urusi kuwa imehusika na mauaji hayo kwa kuandika katika ukurasa wake wa Facebook akisema kuwa serikali ya Rais Putin inahusika moja kwa moja.

 

Lewandowski atamani kuondoka Bayern Munich
Ombi la Rais wa Mali kwa Mamoudou lazua gumzo