Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jimbo la Bunda Bi. Janeti Mayanja amepokea madawati 90 yaliyotolewa na Mbunge wa Jimbo hilo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Bi. Ester Bulaya, ambapo hapo awali  madiwani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika jimbo hilo walikataa kupokea madawati hayo baada ya kuwa yameandikwa  jina la mbunge huyo pamoja na kuwa yamenunuliwa na fedha za Mfuko wa Jimbo.
Akizungumza leo kwa njia ya simu, Mkurugenzi  Mayanja alisema kuwa  amepokea madawati hayo jana  Agosti 12  kutoka kwa Mbunge wa jimbo hilo Ester Bulaya baada ya kufutwa jina lake, ambapo madawati hayo tayari yamewasilishwa katika shule tatu zilikuwa na uhaba.
“Tulifanya kikao na Mbunge Bulaya na tukakubaliana kuwa ni vyema majina yake yakafutwa katika madawati hayo kwa vile yalinunuliwa kwa fedha  za Mfuko wa  Jimbo, lakini endapo mbunge atapenda kutupa madawati atakayonunua kwa  fedha zake binafsi  na kuandika majina yake hapo tutapokea kwa vile bado kuna tunauhitaji katika jimbo letu” alisema Mkurugenzi Mayanja
Alifafanua kuwa fedha zilizotumika kununua  madawati hayo zilikuwa ni  fedha za Mfuko wa  Jimbo zinazotokana na ruzuku ya Serikali ambazo matumizi yake hupangwa na Ofisi ya Mbunge.
Madawati hayo 90 yalisambazwa katika shule tatu za Msingi zilizopo katika Jimbo la Bunda zilizokuwa na uhaba wa madawati  ambazo ni  Nyatwali, Nyerere na Ligamba,  zilizopewa madawati 30 kwa kila moja

Nape ajibu taarifa za kuzuia vyombo vya habari kuripoti maandamano ya chadema
Maalim Seif amtembelea Ndugai nyumbani kwake