Korea Kusini imesema haijapokea mwitikio wowote kutoka Korea Kaskazini kuhusu mkutano kati ya kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong-un na Rais wa Marekani, Donald Trump.

Hali hiyo inakuja wakati ambapo hivi karibuni Rais Trump alikubali mwaliko wa Korea Kaskazini kufanya mazungumzo ya ana kwa ana na kiongozi wa Korea ya Kaskazini kwa ajili ya kumaliza mzozo wa muda mrefu uliokuwepo kati ya nchi hizo mbili.

Taarifa za kina kuhusu muundo wa mazungumzo bado hazijawekwa wazi, huku mahali na ajenda za mkutano huo vikiwa bado havifahamiki.

Wachambuzi wa mambo nao wanaonekana kusita kuzungumzia kile kitakachofikiwa katika mazungumzo hayo kutokana na utata wa mambo yalivyo.

Tayari maafisa wa Korea Kusini waliozungumza na Rais Trump kwa sasa wanaelekea China na Japan kuwafikishia taarifa hizo viongozi wa nchi hizo kuhusu mazungumzo yajayo kati ya Korea Kaskazini na Marekani.

Maafisa wa Korea Kusini wamesema kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong-un amejiandaa kuachana na mpango wa kutengeneza silaha za nyuklia.

Macron na Modi wazindua mfumo wa umeme jua Delhi
Dkt. Mwakyembe awataka maafisa habari kubadilika