Mlipuko uliotokea kwenye tenki la kemikali karibu na uwanja wa ndege wa Cairo, mashariki mji huo mkuu wa Misri na kujeruhi takribani watu 12, kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na jeshi la nchi hiyo jana usiku.

Mashuhuda wa tukio hilo wameeleza kuwa walisikia kelele na kushuhudia mwanga mkubwa wa moto na moshi, kama ambavyo picha zilionekana kwenye mitandao ya kijamii.

Msemaji wa jeshi hilo, Tamer el-Refai aliandika kupitia Twitter, “Ongezeko la joto limesababisha mlipuko ambao ulitokea katika kampuni iliyojikita katika utengenezaji wa kemikali, kwenye eneo linalodhibitiwa na jeshi.”

Shirika la habari la AFP limeeleza kuwa vikosi vya uokoaji viliwasili kwa wingi kwenye eneo hilo ikiwa ni pamoja na magari maalum ya dharura. Majeruhi walikimbizwa hospitalini huku vikosi vikipambana kuudhibiti moto mkubwa.

Katika hatua nyingine, Idara ya Mamlaka ya Anga ilikanusha taarifa za awali kuwa mlipuko huo ulitokea ndani ya uwanja wa ndege.

Msemaji wa Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi, Bassem Abdel Karima amesema kuwa hakuna kilichoharibika ndani ya uwanja huo na kwamba shughuli za usafirishaji zinaendelea kama kawaida.

“Kutua na kuondoka kwa ndege zetu hakujaathiriwa na mlipuko huo wa tenki la kemikali.”

Video: Ngoma mpya ya Diamond Platinumz 'Baila' hii hapa
Aliyetimuliwa na Lugola kikaoni ang'atuka, JPM afanya uteuzi mwingine