Mnada wa Makontena 20 ya mkuu wa mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda umeendeshwa na tayari baadhi ya wateja wamekagua bidhaa kwa ajili ya kununua.

Mkurugenzi Mtendaji  wa Kampuni inayohusika na kuendesha minada ya Yono Auction Mart, Scholastica Kevela, amesema kuwa kuna matumaini ya bidhaa zote kununuliwa tofauti na mnada wa awali uliokosa wateja.

Akiendesha mnada huo Kevela amezitaja bidhaa zilizomo kwenye makontena hayo ni samani za ofisini kama vile viti, meza na makabati, huku bei zilizotajwa ni kati ya Shilingi milioni 6 hadi milioni 15 huku akibainisha kuwa mnada huo umehusisha sio makontena ya Makonda pekee yake bali na makontena mengine ambayo yameshindwa kulipiwa ikiwemo vifaa vya kilimo pamoja na magari.

Aidha, mnada huo umefanyika katika bandari kavu ya Malawi Cargo na wanunuzi wametakiwa kuwa na vitambulisho, leseni ya gari na hati ya kusafiria.

Makontena hayo yanapigwa mnada baada ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, kuagiza makontena 20 ya samani yaliyoingizwa nchini na Makonda, yapigwe mnada ikiwa ni sehemu ya kusimamia sheria na kanuni za kodi zilizopo nchini.

Hata hivyo, mbali na Makonda mwenyewe kutoridhia uamuzi huo wa serikali, tayari Rais Dkt. Magufuli amesema sheria za nchi zinasema wazi kuwa ni mtu mmoja tu katika nchi mwenye dhamana ya kutolipa kodi kwa mujibu wa sheria ya fedha, sheria ya madeni, sheria ya dhamana na ya misaada.

Video: Watoto wa kike ni lazima wasaidiwe ili waweze kutimiza ndoto- Ridhiwani Kikwete
Video: Anna Makinda awafunda wabunge