Mbunge wa Jimbo la Kibamba kupitia chama cha Demokrasia (CHADEMA), John Mnyika amemuomba Rais Dkt. John Magufuli kushughulikia marekebisho ya Katiba kabla ya kuelekea katika uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2020

Ameyasema hayo jijini Dar es salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu majadiliano ya mabadiliko ya kikatiba na kisheria kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 ili kusudi pawepo na chaguzi huru na haki.

“Ili kuepusha nchi yetu isiingie kwenye matatizo ya kisiasa kuelekea mwaka 2020, ushauri wangu na rai yangu kwamba Rais Magufuli ni vyema angekubaliana na makubaliano ambayo Rais mstaafu Jakaya Kikwete aliyaridhia kuhusiana na marekebisho ya Katiba,” amesema Mnyika.

Amesema kuwa bila ya kufanyika mabadiliko hayo bado kutakuwepo na tatizo kubwa ndani ya Tume ya Uchaguzi kwa kushindwa kufanya kazi zao kwa uhuru.

Hata hivyo, Novemba 20, 2016 Jukwaa la Katiba Tanzania (JUKATA) iliitaka serikali ya inayoongozwa na Rais Magufuli ifanye mabadiliko ya msingi katika Katiba kabla ya kuingia kwenye maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao wa Rais na Wabunge wa mwaka 2020.

 

Video: Kauli ya Viongozi wa Dini baada ya kukutana na Rais Magufuli Ikulu leo
JUKATA Yataka wabunge watungiwe sheria