Bilionea Mohammed Dewji amerejea rasmi mtandaoni, siku chache tangu aachiwe huru na watu waliokuwa wamemteka.

Mo ambaye amekuwa mjumbe maarufu kwenye mtandao wa Twitter, akiwa na wafuasi 586, jana aliandika ujumbe wa kwanza tangu tukio hilo pamoja na kuungana na tweet ya rafiki yake, January Makamba (Waziri mwenye dhamana ya Muungano na Mazingira).

Kupitia ujumbe huo, Mo amemshukuru Mungu na watu wote waliomuombea alipokuwa mikononi mwa watesi wake.

“Nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kuokoa maisha yangu. Pamoja na kupitia kipindi kigumu lakini daima amesimama upande wangu. Marafiki zangu, napenda kuwashukuru wote kwa maombi yenu na kunitakia kheri. Mungu awazidishie kwa wema wenu. Baraka za Mungu ziwe nanyi leo na daima,” alitweet.

Kabla ya tweet hiyo, Mo ali-retweet ujumbe wa Makamba kuhusu namna alivyohitajika polisi na kutoa taarifa kuhusu kutekwa kwa Bilionea huyo,akikanusha taarifa zilizodai kuwa alikamatwa.

Mara ya mwisho, Mo alitweet Oktoba 10 ambayo ni siku moja kabla ya kutekwa na watu hao.

Mo alitekwa na watu wasiojulikana katika hoteli ya Colosseum iliyoko Oysterbay jijini Dar es Salaam alipoenda kufanya mazoezi alfajiri, na alipatikana baada ya watesi wake kumtupa katika eneo la Gymkhana jijini humo.

Arsenal yamfuta Unai Emery tope la woga
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Oktoba 23, 2018