Muwekezaji na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba Mohammed Dewji ‘MO’ amewahakikishia mashabiki na wanachama wa klabu hiyo kuwa wamepanga kutomuachia mchezaji yeyote katika dirisha kubwa la usajili la kiangazi lakini pia watamchukua mchezaji yeyote wanayemtaka kama kocha anamwitaji.

Dewji ambaye aliichukua Simba misimu miwili iliyopita, ambapo tangu ameichukua kwa bilioni 20 tayari klabu hiyo imeshaanza kuendeshwa kisasa na matokeo uwanjani yanaonekana sambamba na kufanyika usajili ‘Bab kubwa’.

Mohammed Dewji ameyasema hayo kupitia ukurasa wake rasmi wa Twitter ameandika “Wanasimba wenzangu nataka niwahakikishie hakuna mchezaji wetu yeyote atakayeondoka SIMBA. Lakini pia tutasajili mchezaji yeyote, kutoka popote, kama mwalimu wetu atamuhitaji kwenye kikosi chake, Tutashuka kwa kishindo: hatuna maneno mengi lakini tupo”.

MO anayesema hayo baada ya wachezaji kadhaa wa klabu hiyo kuhusishwa kujiunga na vilabu vingine kama Ibrahim Ajibu ambaye anahusishwa kusajiliwa na timu moja wapo nje za nchi, Clatous Chota Chama na Meddie Kagere alikuwa anahusishwa kwenda Levante. Wakati huo huo Simba pia imekuwa ikitajwa kuwa katika rada ya kuwataka wachezaji kama Shonga, Sarpong, Papy Kabamba Tshishimbi na wengineo.

David Molinga ajitetea safari ya Shinyanga
Hoja zilizotikisa Bunge kumpongeza Rais mapambano dhidi ya Corona.