Siku chache baada ya timu ya WCB na Ali Kiba kufanya matamasha makubwa ya ‘Wasafi Festival’ na ‘Funga Mwaka na Ali Kiba’ kwa nyakati tofauti nchini Kenya, wasanii nchini humo wameanzisha kampeni nzito kwenye mitandao ya kijamii kudai wanachoita haki yao kwenye vyombo vya habari.

Diamond na WCB walitangulia kufanya balaa jijini Mombasa Desemba na kisha Ali Kiba naye alifunika jiji hilo akiufunga mwaka 2018. WCB ilikamilisha mzunguko wake jijini Nairobi ambapo mjadala mkubwa wa ubora wa tamasha hilo ulifanya mtandao wa Twitter kuzizima.

Mafanikio ya wasanii wa Tanzania kwenye majukwaa ya Kenya, mbali na mambo mengine yanadaiwa kutokana na namna ambavyo vyombo vya habari nchini humo vinavyocheza kwa wingi nyimbo zao hata zaidi ya wasanii wa ndani.

Baadhi ya wasanii na mashabiki wa Kenya wameivalia njuga kampeni dhidi ya vyombo vya habari nchini humo ambavyo vinadaiwa kucheza chini ya 30% ya muziki wa ndani ya nchi na kujikita katika muziki wa nje ya nchi yao.

Kupitia Twitter, wengi wamedai kuwa zaidi ya asilimia 70 za nyimbo zinazochezwa nchini Kenya ni Bongo Fleva (Tanzania), Nigeria, Afrika Kusini na nchi za Magharibi, hali inayodidimiza soko la muziki wa nchi hiyo. Hivyo, wameanzisha kampeni yenye Hash Tag ‘Play Kenya Music (Cheza muziki wa Kenya.

Wasanii wa Tanzania kama Diamond, Harmonize na Ali Kiba, ni wasanii wanaofanya vizuri nchini Kenya zaidi ya wasanii wengi wakubwa wa nchi hiyo na matamasha yao hufana zaidi.

Vita hiyo ilimuibua Gavana wa Mombasa, Ali Hassan Joho ambaye aliiunga mkono lakini moto ulimgeukia.

Gavana Joho aliweka picha kwenye Instagram akiwa na Willy Paul na kuandika, ““#PlayKeMusic cc @willy.paul.msafi @gatesmgenge @chris001ke @daddyowen @realshinski @thenaiboi @officialsusumila @jalangoo.”

Moto uliwaka kwenye comments ambapo wengi walimvaa wakidai kuwa aliwahi kumlipa Chris Brown zaidi ya Sh90 milioni za Kenya ili kufanya tamasha nchini humo huku akiwaacha wasanii wa ndani.

“Says someone who brought Chris Brown to Mombasa Kenya and paid him 90Million for an hour’s performance,” aliandika Chanchima Asiago, akimaanisha kuwa “Anasema mtu aliyemleta Chris Brown Mombasa Kenya na kumlipa Sh90 milioni [za Kenya] kwa ajili ya kuimba kwa saa moja.”

Wengine walimvaa kwa kuwapeleka nchini humo wasanii wa Tanzania ikiwa ni pamoja na Ali Kiba na Ommy Dimpoz. Ikumbukwe kuwa Gavana Joho ni rafiki wa karibu wa Ali Kiba.

Gavana wa Mombasa, Hassan Joho akiwa na Ali Kiba pamoja na mwanafunzi kwenye tukio la kijamii

Sehemu ya comments za Wakenya kwa Gavana Joho:

hassandrake: Sasa play Kenya lakini Alikiba na Ommy Dimpoz hawakosi kwa kila event unaorganize, Sultan Vipi?

unado_nini: Kwenda kabisa! Wewe unapenda kuleta alikiba hadi theme ya campaign yako ilikuwa tz music. Nyamazanga saa zingine wanyonge wakiongea. Immoral cantankerousios nyoko.

pmwangi_gitau: Bwana Governor maybe you need to move a step further and not just I.G posts, if only half the cash you have paid to ali kiba could have been given to susumila maybe he could be having his own Wasafi thing going on… Less talk more action could help!

Wengine walitafuta alama za kukosoa na kwenda mbali wakidai jumbe zinazoimbwa kwenye nyimbo kubwa za wasanii wa Tanzania na zinazochezwa hadi kwenye matamasha ya watoto zina ‘mambo ya kikubwa’.

Hata hivyo, baadhi ya wasanii wakongwe kama Collo ambao walikuwa na mtazamo tofauti, wakitaka wasanii kutojikita katika kudai nyimbo zao zichezwe kwa asilimia 100 na badala yake waangalie namna ya kuingiza pesa zaidi.

Collo

“Wasanii wenzangu wa Kenya, hina maana kutaka nyimbo zenu kuchezwa kwa 100% wakati hamlipwi kitu. Ndio maana sishangai wengi wetu wanahangaikia kupata umaarufu bila kujali wana pesa au hawana. Chukulieni nafasi mlionayo kama baraka na muache kuwalaumu watangazaji na MaDJ,” unasomeka sehemu ya ujumbe wa Collo.

Naye Nonini amewachana wasanii wa nchi hiyo ambao hujiweka kando wanapoalikwa kushiriki vikao na mijadala inayolenga kuinua hali ya muziki wa Kenya.

Mtangazaji maarufu, Jalang’o amewataka wasanii kutafuta siri ya mafanikio ya Sauti Sol badala ya kulilia nyimbo zao kuchezwa tu kwa 100%.

Video: Ndege mpya ya sita kuwasili leo
Ronaldo kitanzini tena kwa ubakaji, polisi wataka vipimo vya DNA