Meneja wa Man Utd Jose Mourinho amemtuhumu muamuzi aliyechezesha mchezo wa jana ambao ulishuhudia kikosi chake kikikubali kubamizwa mabao matatu kwa moja dhidi ya Watford.

Mourinho amemtupia lawama muamuzi (Michael Oliver ) kwa kusema hakuitendea haki Man Utd, hasa katika maamuzi aliyoyachukua ya kulikubali bao la kwanza la Watford ambao lilifungwa na Etienne Capoue.

Amesema kabla ya bao hilo kufungwa mshambuliaji wake kutoka nchini Ufaransa Anthony Martial alitendewa makosa ya kukabwa kwa makusudi na Daryl Janmaat ambaye alipiga mpira wa pembeni uliomfikia Capoue na kufunga bao hilo.

“Nimechoshwa na maamuzi yanayotolewa dhidi ya kikosi changu, na hii sio mara ya kwanza,” Alisema Mourinho.

“Siwezi kuongeza lolote la kusema kwa sababu najua sitofanikisha suala la kubadili tabia hii, kama mtakumbuka hata katika mchezo uliopita dhidi ya Man City bado tulitendewa ndivyo sivyo lakini muamuzi hakufanya kazi yake.

“Leo (jana), mnafahamu kilichotokea kabla ya kufungwa kwa bao la kwanza la wapinzani wetu, kwa hiyo tumekua tunaadhibiwa kwa makosa ya watu wengine.”

Kosa ambalo Mourinho amelilalamikia kwa kukumbushia mchezo uliopita dhidi ya Man City, ni lile la mlinda mlango Claudio Bravo kumchezea hovyo mshambuliaji Wayne Rooney katika eneo la hatari, lakini muamuzi Mark Clattenburg aliashiria mchezo kuendelea.

Hatua ya kufungwa kwa Man Utd katika mchezo wa jana, kunaifanya klabu hiyo ya Old Trafford kupoteza mchezo watatu mfululizo kwa kipindi cha siku tisa.

Mabao ya Watford yalifungwa na Etienne Capoue, Juan Camilo Zuniga pamoja na Troy Deeney huku Marcus Rashford akifunga bao pekee la Man utd.

Video: Diamond Platnumz avaa viatu vya Saida Karoli
Prof. Ngowi azungumzia suala la Serikali kuhamia Dodoma