Naibu waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Luhaga Mpina amewapongeza viongozi wa mikoa, wilaya na halmashauri nchini waliotekeleza kwa kiwango cha kuridhisha agizo la kusimamia utekelezaji wa siku ya kitaifa ya kufanya usafi na kuhakikisha usafi wa mazingira katika maeneo yao unaimarishwa.

Ameyasema hayo Wilayani Maswa alipokuwa akishiriki zoezi la kufanya usafi kitaifa na kuongeza kuwa majina ya viongozi hao pamoja na wale ambao wamezembea kutekeleza agizo hilo  yatafikishwa kwa Rais na Makamu kwa hatua za kiutendaji.

“Hatuwezi kufikia mapinduzi ya uchumi wa viwanda kama taifa litaendelea kuwa chafu kwani tutaendelea kupoteza nguvu kazi nyingi kutokana na maradhi yanayosababishwa na uchafu, hivyo viongozi wa mikoa na wilaya wana jukumu kubwa la kusimamia usafi wa mazingira.” Amesema Mpina.

Amesema kuwa serikali imeona kuwa usafi ndio afya na usafi ndio maisha ndio maana Serikali imeitenga siku ya Jumamosi ya mwisho wa mwezi kuwa ni siku maalum kwa ajili ya usafi wa Mazingira.

Hata hivyo, Mpina amebaini changamoto mbalimbali za mazingira zinazoikumba wilaya hiyo ikiwa ni pamoja na  upungufu wa matundu ya vyoo katika soko la Maswa, mazingira yasiyoridhisha ya kufanyia biashara sokoni na ukosefu wa maji katika machinjio ya wilaya. ambapo ameuekeza uongozi wa Halmashauri kuhakikisha ndani ya miezi mitatu wanatatua changamoto ya upungufu wa matundu ya choo na kuwepo kwa mabanda ya kisasa ya kufanyia biashara katika soko hilo.

Kwa Upande wake kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Vivian Christopher, amesema kuwa Halmashauri yake imetenga fedha kwa ajili ya kushughulikia changamoto hizo katika Bajeti wilaya kwa mwaka wa fedha 2017/2018

Mkuu wa mkoa aukingia kifua mgodi wa dhahabu, amchimba mkwara Naibu Waziri
NEC yatoa ufafanuzi kuhusu uteuzi wa wabunge CUF