Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Iringa kimewataka wanachama na wadau wa chama hicho kuupuza ujumbe wa mbunge wa jimbo la Iringa mjini, kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Peter Msigwa kuwa chama hicho kipo imara na sio dhaifu.

Hayo yamesemwa na Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM mkoa wa Iringa, Ramadhani Baraza alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambapo amesema kuwa mbunge huyo anatakiwa kufanya mkutano wa hadhara kuwaaga wananchi wa mkoa wa Iringa kwa kuwa zama za kuiongoza Manispaa ya Iringa umefika kikomo.

“Zama za Msigwa zimeisha kuongoza Manispaa ya Iringa kwa kuwa wananchi wameshamchoka kwa kuwa sio kiongozi aliyewasaidia kuleta maendeleo kwani toka aingie madarakani hajawahi kufanya maendeleo yeyeto yale kwenye jimbo hili la Iringa,”amesema Baraza

Amesema kuwa chama cha mapinduzi kimesema hivyo kwa kuwa kipo imara kutokana na aina ya uongozi walionao na mfumo wa siasa ambao wamekuwa wakiutumia kuwafikia wananchi wa mkoa wa Iringa.

Aidha, Baraza amesema kuwa wapinzani wamekuwa hawana jambo jipya ambalo wanaweza kulitekeleza kwa kuwa serikali ya chama cha mapinduzi kimesimamia vilivyo serikali na kuhakikisha wanatatua changamoto za wananchi waliowapa mamlaka ya kuwaongoza.

Hata hivyo, hoja hiyo imekuja siku kadhaa baada ya mbunge wa jimbo la Iringa kusema kuwa chama cha mapinduzi mkoa wa Iringa ni dhaifu na hakiwezi kumuondoa madarakani labda yeye aamue kung’atuka kwa hiyari yake.

LIVE: Yanayojiri Bungeni Dodoma leo Aprili 24, 2019
Video: Utata ripoti ya IMF, Lema atuma waraka mzito kwa Magufuli