Uwezo wa kufikiri wa kizazi fulani, unaweza kuathiriwa na hali na changamoto wanazopitia wanawake wajawazito katika hatua za kushiriki uumbaji wa mwana aliye ndani ya tumbo lao kwa muda wa miezi tisa.

Mwanamke mjamzito anayekabiliwa na tatizo la msongo wa mawazo kutokana na sababu zozote, huweza kuleta athari ya moja kwa moja kwenye mfumo wa ukuaji wa ubongo wa mwanae.

Hayo yamedhihirika kupitia utafiti uliochapishwa kwenye jarida la Clinical Endocrinology, ambao ulionesha kuwa athari hizo zinaweza kupatikana kwa ujauzito wenye umri wa kuanzia wiki 17.

Utafiti huo ulikuja kama muendelezo wa tafiti za awali kwa binadamu na wanyama ambazo zilionesha kuwa endapo mama mjamzito atakabiliwa na tatizo la msongo wa mawazo, anaweza kusababisha mwanae akawa na uwezo mdogo wa kufikiri (IQ).

Hata hivyo, watafiti hao walieleza kuwa lengo lao sio kuwapa hofu wanawake bali ni kuwatahadharisha kuhakikisha wanakuwa na afya nzuri na kuepuka mambo yanayoweza kusababisha msongo wa mawazo.

Timu ya watafiti ikiongozwa na Professa Vivette Glover wa Chuo cha Imperial cha London (Imperial College London) na wasaidizi wake ambao ni wataalam wabobezi wa afya ya mama na mtoto waliwafanyia utafiti wanawake wajawazito 267 kwa kutumia dawa maalum zinazompa mtu hali sawa na ile ya aliye na msongo wa mawazo.

Profesa Glover aliiambia The Guardian kuwa walitoa dawa hizo kwa kuzingatia hali inayoweza kumpata mtu mwenye msongo wa mawazo wa muda mrefu ambayo ni kuchoka sana na kujisikia mgonjwa.

Hivyo, ni vyema kwa jamii kuhakikisha kuwa ili kuendela kuwa na kizazi chenye uwezo mkubwa wa kufikiria na kuamua mambo, ni vyema tukaanza na kuwajali na kuwapa furaha wanawake wajawazito. Changamoto wanazozipitia katika ngazi za familia zinaweza kuwa chanzo cha kukosa mwana mwenye uwezo wa kuliinua Taifa.

TUCTA Dar waomba serikali 'kuwafikiria' waliofukuzwa kwa vyeti feki
Video: Azma afunguka alivyowachanganya ‘Sugu’ na Izzo B Kwenye Garagasha