Enzi hizi tofauti na zile za zamani ambapo ukimaliza chuo uwezekano mkubwa mtu mmoja kupata ajira katika kampuni zaidi ya tatu, hali hii ni tofauti na sasa kwani zamani wanaofanikiwa kusoma ni wachache kutokana na uhaba wa Taasisi za elimu kulinganisha hivi sasa ambapo kuna wingi wa Taasisi za kutoa elimu  na kila Taasisi ina wanafunzi zaidi ya 1000 jambo ambalo hupelekea ushindani mkubwa hasa katika soko la ajira.

Katika chuo kimoja wanaohitimu ni zaidi ya 3,000 ambapo katika kila kitivo si chini ya wanafunzi 200 bado vyuo vingine vinavyotoa elimu hiyo hivyo inatokea katika ofisi inayohitaji mtumishi mmoja kushika nafasi fulani watu zaidi ya 10,000 wamehitimu fani hiyo.

Zamani ilikuwa mtu aliyemaliza darasa la saba anaonekana mtu wa elimu ya chini lakini hata kwa sasa kutokana na uwingi wa watu kumiliki shahada mbalimbali thamani ya elimu kama shahada na stashada imeonekana kushuka kwa kiwango fulani kutokana kwamba wengi wenye elimu za juu wapo mtaani huku wengine wakijihusha na biashara ndogo ndogo.

Mbali wahitimu kuwa wengi bado kuna tatizo la wahitimu kutokuwa na vigezo vya kuajiriwa kutokana na kukosa kujiamini na kukosa ufanisi wa kazi, bado najiuliza shida ni nini?.

Kwa uelewa wangu mfupi ujasiri uletwa pale mtu anapokuwa na uhakika wa jambo fulani kwa kulijua kiundani, je tafsiri hii inanifanya nielewe kwamba wahitimu wengi bado wanakuwa hawajaiva juu ya utaalamu wao ndio maana wengi wao hata wakiitwa katika usahili wakazi huonekana kushindwa kutetea uwezo wao juu ya taaluma yao, hiyo ni changamoto.

Changamoto nyingine ni kwamba Chuoni mambo mengi yanafundishwa wahadhiri wanajitahidi kwa kiasi chake ila wanakosa mbinu za kuwaandaa vyema wanafunzi wao katika kukabiliana na kazi mara baada ya kuhitimu sababu mwanafunzi ni mwanafunzi mara nyingi wanafunzi huwa ni watu wa kukariri mambo ili waweze kujibu vyema katika mitihani yao kutokana na kwamba vitu amabavyo walimu huuliza katika mitihani yao ni vile vile ambavyo vipo kwenye madaftari yao hivyo ni rahisi kwa mtu aliyekremu na kuotea kufaulu mtihani huo.

Nadhani ifike wakati wahadhiri waandae mbinu za kuwaandaa wanafunzi wao kupambana na ajira kwa kuwajengea ujasiri zaidi, ufanisi na uweledi wa taaluma zao kwani kupitia ujasiri huo wanaweza kuutumia hata katika mambo mengine yakiwemi kujiajiri wenyewe tukiamini kuwa sio kila muhitimu ataajiriwa.

Hakuna uwiano wowote kati ya ajira zinazotolewa na wanafunzi wanaohitimu, hivyo basi naunga mkono hoja inayodai mashuleni kuwepo na masomo ya ujasiriamali ili kuokoa namba kubwa ya watu waliopo mtaani bila shughuli yeyote.

Serikali kwa ujumla inakazi kubwa sana kuhakikisha kweli elimu ni mkombozi wa maisha kwa jamii, toa maoni yako kuisaidia serikali katika kutatua tatizo hilo, kwani ni kweli elimu ni nzuri basi iwe na msaada katika kila leo yetu.

Dkt. Possi awasilisha hati ya utambulisho kwa Papa Francis
Mama Kanumba ampa wakati mgumu Steve Nyerere