Kocha Mkuu wa Young Africans Luc Eymael amewataka wachezaji wa klabu hiyo kupambana kwa kujituma kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mtibwa Sugar, utakaochezwa kesho, Uwanja wa Jamuhuri mjini Morogoro.

Young Africans inayoshika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu kwa kufikisha alama 68 mbili mbele ya Azam FC wanaowafukuzia kwa kasi, itahitaji ushindi ili kuzidi kujihakikishia kumaliza katika nafasi hiyo, lakini Mtibwa Sugar nayo itahitaji ushindi ili kujinusuru na janga la kushuka daraja.

Tayari Young Africans wameshawasili mjini Morogoro, na leo wanatarajiwa kufanya mazoezi yao ya mwisho kwenye uwanja wa Jamuhuri mjini humo, huku taarifa zikieleza kuwa kocha msaidizi Charles Boniface Mkwasa na kocha wa makipa Peter Manyika wameachwa Dar es salaam.

Kocha Eymael amesema wachezaji wake wako vizuri kuelekea katika mchezo huo wa mzunguuko wa 36 wa Ligi Kuu, na anaamini wanaweza kupata ushindi huku akiwataka kuzidisha umakini uwanjani.

Kwa upande wa Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar, Zuberi Katwila, amesema mchezo huo unampasua kichwa kwa kuwa anaamini utakuwa na ushindani mkubwa huku wakihitaji kushinda kutokana na nafasi waliyopo kwa sasa.

Amesema msimu huu kwa upande wao umekuwa mgumu, kutokana na matokeo ambayo hayaridhishi kwenye michezo ambayo wamecheza.

Michezo mingine ya mzunguuko wa 37 Ligi Kuu Tanzania Bara itakayochezwa kesho na keshokutwa ni Singida United dhidi ya Kagera Sugar (Uwanja wa Liti-Singida), Mwadui FC Vs Biashara United (Shinyanga), KMC FC Vs TZ Prisons (Uhuru-Dar es salaam), Mbao FC Vs Namungo FC (CCM Kirumba-Mwanza), Azam FC VS Mbeya City (Azam Complex Chamazi- Dar es salaam), Polisi Tanzania Vs JKT Tanzania (Ushirika-Moshi/Kilimanjaro), Alliance FC Vs Ndanda FC (Nyamagana-Mwanza), Coastal Union Vs Simba (CCM Mkwakwani-Tanga) na Lipuli FC Vs Ruvu Shooting (Samora-Iringa).

Makata kuwasilisha mpango kazi Dodoma FC 2020/21
Simba Queens kuikabili Mlandizi Queens