YANGA SC leo imecheza mechi ya tano bila kushinda hata moja, baada ya kulazimishwa sare ya 0-0 na Mtibwa Sugar ya Morogoro katika mchezo wa kirafiki jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mchezo huo ulikuwa sehemu ya maandalizi ya mchezo wa Kundi A Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Mouloudia Olympique Bejaia ya Algeria Jumamosi ijayo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Yanga itakuwa inasaka ushindi wa kwanza siku hiyo baada ya kucheza mechi zote nne za awali bila ushindi, ikifungwa tatu na kutoa sare moja.

Yanga ilifungwa 1-0 mara mbili, na Mouloudia Olympique Bejaia nchini Algeria na TP Mazembe Dar es Salaam kabla ya kutoa sare ya 1-1 na Medeama SC mjini hapa na baadaye kwenda kufungwa 3-1 na timu hiyo nchini Ghana katika mchezo wa marudiano.

Mara ya mwisho Yanga kushinda ilikuwa ni kwenye Fainali ya Kombe la TFF, ilipoibugiza Azam FC 3-1 Uwanja wa Taifa.

Yanga itahitimisha mechi zake za Kundi A Kombe la Shirikisho kwa kumenyana na wenyeji TP Mazembe ya DRC mjini Lubumbashi Agosti 23, mwaka huu.

Mazembe inaongoza Kundi A kwa pointi zake 10 baada ya mechi nne, ikishinda tatu na kutoa sare moja, ikifuatiwa na Bejaia na Medeama, ambazo kila moja ina pointi tano za sare tatu na ushindi mmoja, wakati Yanga inashika mkia kwa pointi yake moja.

Kikosi cha Yanga kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Hassan Kessy, Mwinyi Mngwali, Andrew Vincent ‘Dante’, Vincent Bossou, Said Makapu, Juma Mahadhi, Thabani Kamusoko, Matheo Anthony/Yussuf Mhilu dk62, Obrey Chirwa na Deus Kaseke.

Mtibwa Sugar; Abdallah Makangana, Ally Shomary, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Salim Mbonde, Cassian Ponera, Henry Joseph, Ally Makarani, Ibrahim Rajab ‘Jeba’/Vincent Barnabas dk76, Rashid Mandawa/Jaffar Salum dk79, Mohammed Issa/Shaaban Nditi dk53 na Haroun Chanongo/Maulid Gole dk87.

 

Serengeti Boys Waivimbia Afrika Kusini
Yusuf Manji Amjibu Mohamed Dewji "Mo"