Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo amelitaka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kutoa leseni kwa wakati kwa kampuni za utafiti wa uchimbaji wa gesi na mafuta nchini.
Muhongo ameyasema hayo Jijini Dar es salaam katika kikao cha majumuisho kilicho wajumiuisha TPDC na kampuni za utafiti za uchimbaji gesi na mafuta nchini na watendaji kutoka Wizara ya Nishati na Madini.
Aidha, Muhongo amesema kuwa kuna utaratibu wa ucheleweshaji wa uhuishaji wa leseni jambo ambalo linakwamisha utendaji wa kampuni hizo na kuzitaka kampuni hizo kutuma maombi ya uhuishaji leseni zao miezi sita kabla ya muda wake kuisha.
“Biashara ya gesi na mafuta duniani inaushindani mkubwa hivyo ni vyema kampuni za gesi kuongeza kasi ya utafiti na watendaji kutoka TPDC na Wizara ya Nishati na Madini waongeze kasi ya utoaji wa leseni”alisema Muhongo.
Hata hivyo, Muhongo amesema kuwa ili Tanzania iwe miongoni mwa nchi zenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025,lazima nishati ya umeme iwe ya uhakika.