Mahakama nchini India imemhukumu muigizaji maarufu nchini humo, Salman Khan, kifungo cha miaka mitano jela baada ya kumkuta na hatia ya kufanya ujangili na kumuua swala paa kinyume cha sheria.

Mahakama ya Jodhpur imetoa hukumu hiyo leo kufuatia kosa hilo ambalo Khan anadaiwa kulifanya mwaka 1998 alipokuwa anatayarisha filamu yake Magharibi mwa jimbo la Rajasthan.

Mbali na hukumu hiyo ya kifungo jela, mahakama pia imempiga faini ya repee 10,000 (sawa na $154). Khan amechukuliwa kupelekwa gerezani muda mfupi uliopita.

Waigizaji wengine wanne waliokuwa naye wakati wa tukio hilo ambao waliunganishwa kwenye kesi hiyo wameachiwa huru.

Khan mwenye umri wa miaka 52 ambaye filamu zake zimevuka mipaka ya Hollywood na kuteka kona nyingi za dunia, anayo nafasi ya kukata rufaa kwenye mahakama kuu.

Hii ni kesi ya nne aliyowahi kufunguliwa muigizaji huyo kwa madai ya kufanya ujangili dhidi ya wanyama pori alipokuwa anatayarisha filamu yake ya Hum Saath Saath Hain, mwaka 1998.

Heche aswekwa mahabusu
Ndugai ajibu hoja ya kuundwa kwa tume ya kuchunguza matukio ya uhalifu nchini