Aliyekuwa msanii wa maigizo ya filamu za bongo ambaye aliamua kuachana na mambo ya kidunia na kumrudia Mungu kufuatia mapito mengi aliyopitia, Rose Nungu maarufu kama MunaLove amefunguka mambo mengi kuhusiana na maisha yake kabla na baada ya wokovu wake ambapo moja ya mambo aliyoyazungumza ni kufuatia tabia aliyokuwa yake ya kwenda kwa waganga wa kienyeji kila wiki ili aweze kufanikisha kimaisha.

”Kwa mganga nimeshapelekwa sana tu, sababu nimekutana na watu tofauti, lakini pia nishakuwa na sehemu ya watu kila wiki ni lazima kwa mganga yani kila wiki bila mganga maisha hayaendi, kwahiyo hivo vitu nilijaribu kuvunja yale maroho yakiganga”. Amesema Muna.

Akizungumza na Zamaradi Mketema mtangazaji alipofanyiwa mahojiano kwenye chaneli ya Zamardi TV, Muna amefunguka mambo mengi ambayo watu wengi walikuwa hawayafahamu kuhusu maisha yake ikiwemo namna ambavyo alikuwa anashiriki kwenda kwa waganga, kuvunja ndoa za watu na kugombanisha watu ikiwa pamoja na kuwaliza wanawake wenzake.

Katika mahojiano hayo Muna amesema kuwa huenda kufuatia kifo cha mwanae mpendwa Patrick imekuwa ni pigo kubwa lililomfanya kubadilisha kabisa mwenendo wa maisha yake amesema huenda Mungu alimpitisha katika pito hilo kufuatia dhambi alizokuwa akitenda kabla ya kuokoka.

Lakini pia ameelezea maisha yake baada ya kuokoka akidai kuwa amekuwa ni mtu wa sala mambo yake yote anayafanya akimwamini Mungu na akimuomba Mungu awezee kumuongoza katika kila jambo kwani alipopata matatizo ya kufiwa na mtoto wake watu wake wote wa karibu walimtenga na kumuacha ahangaike peke yake jambo ambalo linamfanya kila leo azidi kumtumikia Mungu kwani ndiye kimbilio lake.

”Mara ya mwisho baada ya kuomba sana nilitokewa na chale kubwa tu kwenye paji la uso” amesema Muna.

Aidha ametoa ushauri kwa wanawake, vijana ambao bado wanaamini mafanikio yanapatikana kwa waganga wa kienyeji, amesema kuwa waganga hakuna kitu wanafanya zaidi ya kucheza na akili za watu wenye shida na matatizo wanaohitaji msaada.

”Awe msichana, mama au kijana, vijana wengi sasa ndio wanakimbia  kwa waganga, waganga ni kama tu sehemu ambayo wanacheza na akili yako sio kwamba wanafanya kile kitu ambacho unakidhamiria, sababu hata mimi nilikuwa naenda lakini vingine havitokei, muda mwingine ni zile husttle zako na wewe unaamini ni zile dawa ambazo ulitumia” Ameshauri Muna.

Amewaomba watu kumwamini Mungu na kumkabidhi maisha yao, kuacha dhana ya kuwategemea waganga katika mambo yao yote.

”Ni vyema kuongea na Mungu katika kila jambo ambalo unataka ulifanye Mungu ndiye atakayeongoza mambo yako, ukimwambia Mungu anakupa kwa wakati hata hutumii nguvu, Mungu anajua unataka nini, anakupa na kukuongezea zaidi ya kile ulichoomba” Amesema Muna.

 

 

Video: Jinsi Vanessa na mpenzi wake mpya wanavyomtesa Jux
Makonda: Ubungo hatujapata viongozi wa maendeleo, bali wa matumbo yao