Rais wa Uganda, Yoweri Museveni amesema kuwa hakuna nchi nyingine duniani iliyoweza kuwa na uchumi unaokua haraka kama Uganda, ukitoa Ujerumani, lakini juhudi za kuleta maendeleo Uganda zinakwamishwa na idadi kubwa ya mafisadi serikalini na wanasiasa wa upinzani.

Amedai kuwa kama Uchumi wa Uganda ungeendelea kukua kwa kasi hiyo, hivi leo ingekuwa tajiri hata kuliko Marekani, ambapo amesema ndoto yake ya kuitajirisha Uganda bado iko hai, akiongeza kuwa hivi sasa, kuna wimbi la wawekezaji wanaoingia nchini humo kwa wingi.

Katika hotuba yake kwa taifa, kabla ya kumalizika kwa mwaka wa fedha 2018/2019, ameeleza kuwa kwasasa, Uganda ingekuwa miongoni mwa nchi mbili tajiri zaidi duniani, lakini ufisadi, uongozi mbaya uliomtangulia, siasa za upinzani na kukosa kutekeleza miradi muhimu kwa wakati, vimefanya nchi hiyo kubaki katika orodha ya nchi masikini.

“Hakuna nchi yoyote ya Ulaya hata Marekani ambayo uchumi wake ulikua kwa kasi kama Uganda kwa muda wa miongo mitatu, isipokuwa Ujerumani ambayo kati ya mwaka 1950 na 1980 kwa asilimia 3.8,” amesema Museveni

Aidha, sekta za viwanda, mafuta na gesi, utalii, nishati, ujenzi wa barabara, reli ya kisasa SGR, na kilimo ndio masuala muhimu ambayo Museveni anaamini nchi yake inastahili kuyatizama kwa umakini zaidi, akiahidi utafiti wa kipekee unaofanywa na wanasayansi wake, wa kuhakikisha kwamba kupe wanakufa wenyewe wanapofyonza damu ya ng’ombe na mifugo wengine.

Hata hivyo, katika hotuba yake, Museveni hakuacha kuwashambulia wapinzani wake, hasa chama cha DP, ambacho kimeonekana kuwavutia wanamziki maarufu, Bobi Wine na Jose Chameleon ambaye amekiacha chama cha Museveni cha NRM.

LIVE IKULU: Rais Magufuli akizungumza na Wafanyabiashara leo Juni 7, 2019
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Juni 7, 2019