Mwanafunzi wa kidato cha Nne wa shule ya sekondari ya Rau iliyopo Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro Emmanuel Tarimo (18), amejinyonga hadi kufa baada ya kudaiwa kuhojiwa na walimu wake kwa zaidi ya saa tano, akituhumiwa kujihusisha kimapenzi na mwanafunzi mwenzake wa kidato cha kwanza.

Kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro, ACP Hamis Issa amethibitisha kutokea kwa tukio hilo kati ya majira ya saa nne za usiku nyumbani kwao.

Aidha, sababu kubwa inayotajwa kusababisha kifo cha mwanafunzi huyo ambaye anajiandaa kufanya mitihani ya kuhitimu kidato cha nne mwaka huu ni kuhusishwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanafunzi mwenzake katika moja ya ofisi ya walimu iliyokuwa wazi shuleni hapo.

Mkuu wa shule hiyo, Nyoni Njinjinji amekiri kuhojiwa kwa mwanafunzi huyo na walimu kuhusiana na tuhuma za kujihusisha kimapenzi na mwenzake ambapo baada ya kukataa, alielekezwa kujieleza kwa barua na alipomaliza aliondoka na kuelekea nyumbani badala ya kuingia darasani.

Hata hivyo, kwa upande wa mama mdogo wa marehemu, Teddy Maro na baadhi ya wanafunzi kwa nyakati tofauti wameeleza kusikitishwa kwao na kifo cha mwanafunzi huyo, huku wakiwasihi walimu kutojenga tabia ya kuwasukuma wanafunzi kukiri kosa ambalo huenda linaweza kuwa si kweli na likawaathiri kisaikolojia.

 

LIVE: Yanayojiri Bungeni Dodoma leo Septemba 6, 2018
Video: Kishindo cha JPM, Makonda achokwa, hakuna Dar ya Makonda