Mwanamke aliyepotea kwa takribani wiki moja baada ya kukodi taxi akielekea hospitalini, amekutwa akiwa amekufa na mwili wake ukiwa na majeraha jijini Nairobi nchini Kenya.

Familia ya mwanamke huyo aliyetajwa kwa jina la Mildred Odira imeeleza kuwa imeukuta mwili wake ukiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti, Jumatatu asubuhi.

Kaka wa marehemu ameiambia Citizen TV kuwa mwili wa ndugu yake ulikuwa na majeraha ya kushambuliwa na kitu chenye ncha kali shingoni na kichwani.

Alisema kuwa wamebaini kuwa watesi wa ndugu yao walivunja miguu yake kwa kuikanyaga na gari.

“Tunajiuliza, nini hasa ambacho Mildred aliwafanyia watu hawa… ni deni la aina gani ambalo sisi kama familia tungeshindwa kulilipa hadi wamfanyie mauaji haya ya kikatili? Alihoji kaka yake.

Mildred Odira ambaye ni mama wa mtoto mmoja na mwajiriwa wa kampuni ya Foresight alipotea tangu Januari 29, baada ya kukodi taxi akielekea hospitalini.

Kufuatia tukio la kupotea kwake, polisi wameshawakamata watuhumiwa kadhaa ikiwa ni pamoja na dereva wa taxi.

Polisi wa Kasrani wameviambia vyombo vya habari kuwa walimkamata dereva huyo Jumamosi baada ya kuonekana kwa mara ya mwisho kwenye CCTV kamera akiwa na Mildred.

Ommy Dimpoz afunguka ya moyoni, Jokate & Jux wampa neno
Taharuki bungeni: Wabunge wakimbia, mwenyekiti asitisha kikao