Mwalimu wa mazoezi maarufu kama Zola D, amemshukia Mlinzi wa Diamond Platnumz, Mwarabu Fighter akidai kuwa amemuingiza kwenye matatizo akishindwa kulipia gharama za huduma aliyomuwekea dhamana.

Zola D amesema kuwa alimuunganisha Mwarabu Fighter na mmiliki wa eneo lake la kufanyia mazoezi (Gym), aliyempa nafasi ya kufanyia sherehe yake ya kumbukumbu ya kuzaliwa (birthday party) kwa makubaliano ya kulipa gharama za kila atakayeogelea kwenye bwawa la kisasa, lakini baada ya kukamilisha shughuli yake alipotea na kuzima simu.

Amesema kuwa tofauti na walivyokubaliana, Mwarabu alitoweka akiacha deni la sh 1,000,000 huku akiwa hajawalipa pia wasaidizi wake kadhaa.

“Mwarabu alipotea kama one week, sasa mimi pale ofisini kwangu wakawa wananipigia simu wananistress ‘Zola vipi’. Yeye wakimpigia simu anawaambia ‘ongea na Zola’. Sasa mimi issue hainihusu, birthday ilikuwa yako umealika watu na umeanza kupost na unaniambia mimi niwalipe, inakuwaje niwalipe mimi?” alisimulia.

“So Mwarabu akawa anaanza kukimbiakimbia, nikimpigia simu hapokei. Mimi nikawa nakasirika, nikamtumia ujumbe nikamwambia ‘Mwarabu unajua nikikasirika wanasemaga Zola mkorofi, anapigaga watu. Nikikasirika ujue mimi ni mwalimu wako halafu tunaheshimiana nitakuja kukuharibia halafu itakuwa matatizo,” aliiambia Wafasi TV.

Hata hivyo, siku chache baadaye, Mwarabu alipata ajali ya pikipiki na kulazwa hospitalini. Hivyo, Zola D ameeleza kuwa amepanga kumtembelea amjulie hali hata kama bado amemkasirikia kwa kitendo hicho.

Mwarabu Fighter amekuwa akifanya mazoezi kwenye gym ya Zola D, chini ya ukufunzi wake na wamekuwa marafiki kwa kipindi kirefu wakiweka picha za pamoja kwenye mitandao ya kijamii.

Urafiki wao sasa uko hatarini kutokana na kukosa uaminifu kwenye makubaliano ya kifedha.

Lennox Lewis awatolea uvivu A. Joshua, Deontay Wilder
Ridhiwani: Mambo yamebadilika, sio kama enzi za JK (Video)