Tangu alipoitikisa himaya ya bongo fleva na ‘Hao’ akiwa na Chid Benz hadi leo amesimama na ‘Bado’ akiwa na BillNass, Mwasiti ameweka wazi kwanini ‘kolabo’ na wasanii wa kike imekuwa adimu kwake.

Mwasiti amesema kuwa uamuzi wake wa kufanya kolabo nyingi na wasanii wa kiume kwanza unatokana na ukweli kuwa anaweza kuwavuta mashabiki wa kike na wa kiume kwenye wimbo wake wa mapenzi wenye mchanganyiko wa sauti na jumbe za wote, lakini kuna zaidi…!

Akizungumza na East Africa TV, Mwasiti amesema kuwa kuna ugumu kuwashirikisha wasanii wa kike wa Tanzania kwa sababu huwa na mambo mengi (complicated) wakati wa kufanya kazi.

“Kama mnapotaka kufanya video anakuwa anataka hata akuzidi wewe… anasema bado hiki bado kile. Lakini kwa watoto wa kiume, ni haraka akiwa na koti lake ametupia na jeans basi,” alisema Mwasiti.

Kwa ufupi, mbali na usumbufu huo, ongezeko la gharama za mahitaji ya wasanii wa kike limejificha ndani ya sababu hiyo kwani mwenye wimbo ndiye anayehusika na gharama zote.

Aliongeza kuwa sababu za wasanii wa kike kutoshirikishana kwa wingi zimekuwa zikitajwa mara kwa mara na wasanii hao kwenye vyombo vya habari na ndivyo zilivyo, huku akikataa kuzirudia.

Boko Haram waigeuka Serikali wakiwa mezani, waua 15
Israel kuwagawa wahamiaji kutoka Afrika