Jeshi la Polisi Mkoani Njombe limelazimika kutumia mabomu ya machozi ili kutawanya mamia ya wananchi waliokuwa wameanza kumshambulia kijana mmoja ambaye jina lake halikufahamika aliyedaiwa kuwa mwizi wa fedha kwa njia ya mitandao.

Tukio hilo limetokea katika Mtaa wa Idundilanga wilaya ya Njombe mkoani humo, ambapo mwizi huyo anadaiwa kukamatwa katika duka linalotoa huduma za mitandao ya pesa kwa njia za simu linalomilikiwa na Cecilia Mwalongo ambapo aliingia ndani ya duka hilo na kuuliza kama anaweza kutoa fedha nyingi lakini hakutaja kiasi.

Akizungumzia tukio hilo, Cecilia amesema kuwa alifanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo wa wizi, baada ya kujiridhisha kuwa ndiye awali aliyewahi kumuibia fedha kiasi cha shilingi milioni 2.9 kwa njia ya mtandao.

Amesema kuwa baada ya kuibiwa fedha hizo aliamua kwenda kutoa taarifa kwa Wakala wa huduma za M-pesa kutoka mkoani Njombe, Ezron Kikoti ambaye alimfundisha jinsi ya kumtambua mwizi wa mtandao.

“Huyu mwizi alikuja mara ya kwanza asubuhi akauliza kama anaweza kutoa fedha nyingi nikamwambia inawezekana akaondoka akasema nisubiri kidogo, akarudi amebadilisha tisheti lakini mimi nikawa nimemkumbuka ingawa sikutaka kumwangali usoni,”amesema Cecilia

Aidha, amesema alipokrudi kwa mara ya pili dukani hapo alisema anataka kutoa fedha kiasi cha shilingi laki 6 ndiyo akatoa kwa mfumo ule wa wizi ambao aliutumia wiki mbili zilizopita.

Hata hivyo, ameongeza kuwa baada ya zoezi lake kukamilika aliangalia ile meseji kama alivyofundishwa na kubaini kuwa yule alikuwa mwizi wa mtandaoni.

 

Wananchi mkoani Njombe watakiwa kufuga Ng'ombe
Video: Polepole amlipua Zitto, amtaka aache kudanganya umma