Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Watu wenye Ulemavu, Stella Ikupa ameviasa Vyama vya Watu wenye Ulemavu nchini kuhakikisha wanashirikiana na Serikali katika kuendeleza ustawi wa Watu wenye Ulemavu.

Ameyasema hayo alipofanya ziara Mkoani Dodoma kukagua utekelezaji wa masuala ya Watu wenye Ulemavu ndani ya mkoa huo, ambapo alikutana na viongozi Mkoa na Vyama vya Watu wenye Ulemavu.

Amesema kuwa ushirikiano baina ya Serikali na vyama vya watu wenye ulemavu ni muhimu katika kuhakikisha haki na masilahi ya watu wenye ulemavu yanalindwa kwa kuzingatia Sera, Sheria na Miongozo mbalimbali.

“Serikali imeendelea kuchukua hatua na kutekeleza jukumu lake la kuhamasisha na kuwalinda watu wenye ulemavu nchini kwa kuhakikisha haki za kundi hilo maalumu zinatekelezwa,” amesema Ikupa

Aidha, ameusisitiza uongozi wa Mkoa huo kuhakikisha unahusisha mahitaji maalumu ya wenye ulemavu katika bajeti wanazozitenga, kutoa elimu na taarifa juu ya upatikanaji wa dawa, mafuta ya watu wenye ualbino na vifaa saidizi, na uundwaji wa kamati za kuhudumia wenye ulemavu.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Edward Mpogolo ameunga mkono na kuyapokea maelekezo yote ya Naibu Waziri na kumhakikishia kuwa Mkoa wa Dodoma utakuwa mstari wa mbele katika kutekeleza maagizo aliyoyatoa.

Naye Katibu wa SHIVYAWATA Mkoa wa Dodoma, Justus Ng’wantalima amempongeza Naibu Waziri kwa jitihada ambazo amekuwa akizifanya katika kutetea Watu wenye Ulemavu.

Video: Fahamu namna tofauti mataifa haya yanavyosherekea 'Valentines Day'
Zitto akumbuka ugomvi wake na Lissu, ‘alisema tumemwaga sana damu zetu’