Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Nape Moses Nnauye ameeleza kuwa Sheria ya Huduma za Habari ya Mwaka 2016 ipo kwa ajili ya manufaa ya kuendeleza sekta ya habari, wana taaluma na Taifa kwa ujumla.
Hayo ameyasema leo Jijini Dar es Salaam alipokutana na Balozi wa Denmark nchini Einar Jensen ambapo aliuliza kuhusu malalamiko ya waandishi wa habari kupoteza ajira kufuatiwa kuwepo kwa sheria hiyo.
Nape alifafanua kuwa sheria hiyo imetoa kipindi cha muda wa miaka mitano kwa wanahabari wasiokuwa na shahada ya kwanza kuweza kujiendeleza kimasomo ili kukidhi sifa za mwandishi wa habari.
“Sheria hii tayari imeshasainiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ambapo kwa sasa tupo katika utaratibu wa kuweka kanuni mbalimbali ili kufidia sehemu zenye mapungufu” alisema Nape
Naye Balozi wa Denmark Nchini Einar Jensen ameipongeza Serikali kwa hatua hiyo nzuri na kuomba ofisi ya Ubalozi wa Denmarm kupatiwa nafasi ya kuweza kukutana na Waziri kwa ajili ya kupata elimu kwa kina kuhusu sheria hiyo.