Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amekiagiza chuo kikuu cha Dar es salaam (UDSM) na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kuwarejesha wanafunzi wote waliofutiwa usajili.

Ndalichako amesema kuwa bado nafasi zipo chuoni hapo hivyo wanafunzi wote waliofutiwa usajili warejeshwe.

Amesema hadi kufikia leo saa 8 anataka zoezi hilo liwe limekwishakamilika kwani atafika chuoni hapo kufuatilia suala hilo.

“Nimemwambia mtendaji Mkuu wa TCU Prof. Kihampa akae na Mkuu wa Chuo ahakikishe wanafunzi waliokuwa wameondolewa warudishwe” Ndalichako.

Waziri amesema hayo kufuatia wanafunzi zaidi ya 600 kufutiwa usajili wa chuo kikuu cha Dar es salaam.

Prof. Ndalichako amesema hayo leo jijini Dar es salaam wakati akifungua mafunzo ya uandaaji wa hesabu za serikali kwa watumishi walioko chini ya wizara yake.

Aidha amesema kuanzia Novemba 1, mwaka huu Serikali itawafikisha kwenye vyombo vya sheria  wahasibu walioghushi nyaraka na kuchezea mifumo ya malipo ya serikali.

Waziri Makamba kitanzini sakata la 'Mo Dewji' kutekwa
Trump azidi kuivimbia Urusi