Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai amesema kuwa atamuandikia barua Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (NEC) kuhusu kujiuzulu kwa aliyekuwa mbunge wa jimbo la Ukonga, Mwita Waitara ili aweze kuendelea na taratibu zingine.

Katika taarifa iliyotolewa na mtandao wa kijamii wa Bunge, imesema kuwa, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepokea rasmi barua ya kujiuzulu ya Mwita Waitara.

“Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai amesema kuwa leo asubuhi amepokea barua ya kujiuzulu Ubunge wa Jimbo la Ukonga kutoka kwa Mhe. Mwita Waitara na hivyo atamwandikia barua Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ili aweze kuendelea na taratibu zingine,”imesema taarifa hiyo

Aidha, Waitara anakuwa Mbunge wa pili CHADEMA, kujivua ubunge ambapo Mbunge wa kwanza alikuwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel ambaye Disemba 14, 2017 alitangaza kujivua rasmi uanachama wa Chama hicho na kujiunga na CCM kwa madai ya kuunga mkono utendaji ya Rais Dkt. Magufuli.

Hata hivyo, kwa kipindi cha miaka mitatu tayari wabunge wanne wameshajivua nyadhifa zao, ambapo dimba lilifunguliwa na Lazaro Nyalandu kutoka CCM kwenda CHADEMA, Maulid Mtulia CUF kuelekea CCM, Godwin Mollel CHADEMA kwenda CCM na sasa Waitara kutoka CHADEMA kuhamia CCM.

Video: Kuna viongozi ndani ya Chadema wananichafua- Kubenea
Mnangagwa amnyang’anya Mugabe walinzi