Kufuatia kifo cha aliyekuwa Diwani wa Viti Maalumu katika Halmashauri ya jiji ya Mbeya kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Ester L. Mpwiza, Tume ya Uchaguzi katika kikao chake cha tarehe 23 Februari, 2018 imemteua Jane Japhaly Jojo kushika nafasi hiyo.

Maamuzi hayo ni kulingana na matakwa ya kifungu cha 86A cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292.

Uteuzi huu umefanyika baada ya kupokea taarifa kutoka kwa Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa ambaye kwa mujibu wa kifungu cha 13 (1) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292, aliitaarifu Tume ya Taifa ya Uchaguzi uwepo wa nafasi hiyo wazi baada ya kifo cha aliyekuwa Diwani wa Viti Maalum kupitia CHADEMA Ndugu Ester L. Mpwiza.

Tume baada ya kupokea Taarifa hiyo, ilikifahamisha Chama cha Demokrasia na Maendeleo Demokrasia ambacho kiliwasilisha jina la mpendekezwa wa kushika nafasi hiyo ambapo jina hilo limetoka katika orodha ya majina yaliyowasilishwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi mwaka 2015.

Taarifa hii imetolewa leo, Februari 26, 2018 na Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Ramadhani Kailima.

 

 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha apata ajali mbaya
Mambosasa: Huyu anafanya vitendo vya unyang'anyi kwa kutumia nguvu kwa wanawake