Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Semistocles Kaijage amesema uchaguzi mdogo katika jimbo la Arumeru Mashariki ni Mei 19, 2019.

Jaji Kaijage ameitangaza tarehe hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 31, 2919 mkoani Morogoro.

Amesema kuwa tume ilipokea barua kutoka kwa Spika wa Bunge la Tanzania ambaye kwa kuzingatia kifungu cha 37(3) cha sheria ya taifa ya uchaguzi aliitaarifu Tume  kuwepo kwa nafasi wazi ya ubunge katika jimbo hilo.

“Nafasi ya jimbo la Arumeru ipo wazi na imetokana na aliyekuwa mbunge Joshua Samwel Nassari kupoteza sifa ya kuwa mbunge kutokana na kutohudhuria mikutano mitatu ya Bunge mfululizo bila ruhusa ya Spika,” amesema Jaji Kaijage.

Aidha, Jaji Kaijage amevitaka vyama vya siasa na wadau wote wa uchaguzi kuzingatia sheria, kanuni, maadili ya uchaguzi, taratibu, miongozo na maelekezo ya uchaguzi wakati wa kipindi cha uchaguzi mdogo.

Machi 14, 2019 Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai alimuandikia barua Mwenyekiti wa NEC, Jaji Kaijage kumtaarifu jimbo la Arumeru Mashariki lipo wazi kutokana na kutohudhuria vikao vya mikutano mitatu mfululizo.

Spika alitaja mikutano hiyo kuwa ni ule wa 12 wa Septemba 4 hadi 14 mwaka 2018, mkutano wa 13 wa Novemba 6 hadi 16 mwaka 2018 na mkutano wa 14 wa 29 Januari hadi Februari 9 mwaka 2019.

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Aprili 1, 2019
Makonda amponda Pierre, Kigwangalla na Jokate wajitokeza "maisha ndiyo haya haya!"