Baada ya kutokea malalamiko kutoka kwa Baraza Kuu la Taifa la Chama cha Wananchi (CUF) kufuatia uteuzi wa wabunge wa viti maalum wa chama hicho, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetoa ufafanuzi dhidi ya uteuzi huo.

Imesema kuwa imesikitishwa na kushangazwa na taarifa ya Baraza la Kuu la Taifa la chama hicho kusema kuwa tume hiyo imekiuka kanuni zake katika uteuzi wa wabunge wanane wa chama hicho ya kujaza nafasi zilizoachwa wazi hivi karibuni na wabunge waliofukuzwa uanachama.

Aidha, NEC imesema kuwa chama husika kilipewa fursa ya kupendekeza majina kabla ya tume hiyo kuanika hadharani majina ya wabunge hao katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katika taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa NEC, Ramadhan Kailima kujibu tuhuma zilizotolewa na CUF na kusambazwa katika mitandao ya kijamii, imesema kuwa katika kanuni iliyojiwekea NEC katika uteuzi wa watu wa kujaza nafasi hufuata mpangilio wa majina.

“Chama husika ndicho huwa kinajua ni nani siyo mwanachama wa chama hicho kwa kipindi cha kujaza nafasi zilizoachwa wazi inapokuwa imetokea lakini siyo tume, hivyo malalamiko kutoka Baraza Kuu la Taifa CUF, yanashangaza,”amesema Kailima.

Hata hivyo, Kailima amesema kuwa taarifa zinazosambazwa katika mitandao ya kijamii zikihusisha NEC kukihujumu chama hicho si za kweli na zinalengo la kupotosha jamii katika utekelezaji wa kazi za Tume.

Mpina anena mazito kuhusu wakuu wa mikoa na wilaya
DAWASCO kuzima mtambo wa Ruvu Juu kwa saa 8