Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom inayowakutanisha watani wa jadi kati ya Simba SC dhidi ya Young Africans itachezwa kesho katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam kuanzia majira ya saa 10 kamili jioni kwa saa za Afrika Mashariki.

Milango ya uwanja wa Taifa itafunguliwa saa 5 kamili asubuhi ili kutoa nafasi kwa wapenzi, wadau na washabiki kuanza kuingia mapema uwanjani.

Tiketi za mchezo huo zimeshaanza kuuzwa leo Ijumaa asubuhi katika vituo vya Karume – Ofisi za TFF, Buguruni – Oilcom, Dar Live – Mbagala, Uwanja wa Taifa, Luther House – Posta, Ferry – Kivukoni, Mnazi Mmoja, Ubungo – Oilcom na Makumbusho – Standi ya mabasi ya daladala na Break Pointi – Kinondoni makabaruni.

Viingilio vya mchezo huo ni shilingi Elfu Thelathini (30,000) kwa viti vya VIP A, Elfu Ishirini (20,000) kwa viti vya VIP B & C, huku kiingilio cha shilingi Elfu Saba (7,000) kikiwa ni kwa viti vyenye rangi ya Blu, Kijani na Orange.

TFF inawaomba wapenzi, wadau na washabiki wa mpira wa miguu nchin kununua tiketi katika magari yaliyopo kwenye vituo vya kuuzia tiketi ili kuondokana na kuuziwa tiketi zisizo sahihi.

Aidha pia TFF imewataka wapenzi, wadau na washabiki wa mpira wa miguu nchini kutovaa mavazi yenye kuashiria/muelekeo wa kisiasa wanapokuja uwanjani kwa kuvaa mavazi yasiyofungamana na masuala hayo.

Mchezo huo utachezeshwa na mwamuzi wa kimataifa mwenye beji ya FIFA, Israel Nkongo (Dsm) akisaidiwa na Josephat Bulali (Tanga), Ferdinand Chacha (Mwanza) mwamuzi wa akiba Soud Lila (Dsm) wakati kamisaa wa mchezo huo atakua Charles Mchau kutoka Kilimanjaro.

Michezo mingine ya Ligi Kuu ya Vodacom siku hiyo ya Jumamosi itakua ni kati ya Coastal Union dhidi ya Mwadui FC katika uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, Maafande wa jeshi la Magereza (Tanzania Prisons) watawakaribisha maafande wa Mgambo Shooting katika uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

Maafande wa JKT Ruvu watakuwa wenyeji wa Stand United katika uwanja wa Karume jijini Dar es salaam, huku wakata miwa wa Turiani Mtibwa Sugar watawakaribisha Majimjaji ya Songea katika uwanja wa Manungu wakati Kagera Sugar watakuwa wenyeji wa Toto Africans katika uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.

Ligi hiyo itaendelea siku ya Jumapili kwa michezo miwili ambapo waoka mikate wa Azam FC watawakaribisha Mbeya City katika uwanja wa Chamazi Complex, huku African Sports wakiwa wenyeji wa Ndanda FC kwenye uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

SSC Napoli Kumsaidia Jese Rodriguez Wa Real Madrid
FA Kuchunguza Uharibifu White Hart Lane