Nigeria ambayo ni moja kati ya nchi zenye nguvu zaidi kiuchumi barani Afrika imesema itasaini makubaliano ya kuifanya Afrika kuwa eneo huru la biashara, katika kikao kijacho cha nchi za Umoja wa Afrika.

Nigeria ilikuwa miongoni mwa nchi ambazo hazikuwa zimesaini makubaliano hayo na uamuzi wake ilioutoa jana ni hatua kubwa kwa mpango huo wa kuondoa tozo na ushuru kwenye mipaka ya nchi hizo.

Makubaliano ya Biashara Huru Barani Afrika (AfCFTA) yamelenga kufungua mipaka kwa ajili ya nchi wanachama wa Umoja wa Afrika waliosaini, hatua inayofungua soko la watu bilioni 1.2.

Mbali na Nigeria, nchi za Eritrea na Benin ndio nchi zilizoweka msimamo kuwa hazitasaini makubalinao hayo.

Rais wa Nigeria, Muhammadu Buhari amesema kuwa nchi yake itaruhusu bidhaa za nchi jirani zenye bei nafuu kuingia nchini kwake na kwamba atazihamasisha nchi nyingine pia zilizokuwa zinasita kuchukua hatua hiyo.

“Msimamo wetu ni rahisi, tunaunga mkono biashara huru ili mradi tu itakuwa ya haki na itafanywa kwa kuzingatia misingi ya usawa,” Tweet inayomkariri Rais Buhari imeeleza.

Nigeria inatarajia kusaini makubaliano hayo kwenye mkutano ujao wa Umoja wa Afrika utakaofanyika Niamey nchini Niger. Makubaliano hayo yalianza rasmi kutekelezwa Mei 30, 2019.

Wakuu wan chi 44 walikutana mwaka jana Kigali nchini Rwanda ambapo walisaini makubaliano hayo.

Wachimbaji wawili wafariki dunia kwa kufukiwa na kifusi
Balozi wa China nchini Uingereza ahojiwa