Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa imetoa dhamana kwa Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi nchini Abdul Nondo, aliyekuwa akishikiliwa na jeshi la polisi tangu Machi 7 Mwaka huu.

Kupitia Wakili wa Mwenyekiti huyo ambaye pia ni Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam, Jebra Kambole amesema kuwa Mahakama hiyo imetoa dhamana kwa masharti ya wadhamini wawili mmoja akiwa mtumishi wa serikali na wote wawe wakazi wa Iringa.

Aidha ameongeza kuwa mbali na masharti hayo Wadhamini wanapaswa kusaini bondi ya kauli Tshs Mil 5.

Kesi ya Abdul Nondo itasikilizwa tena mahakamani  ifikapo Aprili 10, 2018.

Nondo anashtakiwa kwa makosa mawili ambapo kosa la kwanza ni kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni kuwa yupo hatarini akiwa katika eneo la Ubungo na kuzisambaza kwenye mtandao wa Whatsapp.

Kosa la pili limetajwa kuwa ni kutoa taarifa za uongo kwa mtumishi wa umma Mafinga wakati alipokuwa akitoa taarifa katika kituo cha polisi mjini humo kwa kusema kuwa alitekwa na watu wasiojulikana.

Video: ''Anachofanya Ebitoke ni cha kawaida sana'' Blackpass
Gambo awashauri Chadema kushirikiana na Serikali